Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

PlanRep Kuimarisha Mawasiliano Serikalini
Sep 02, 2017
Na Msemaji Mkuu

Na: Frank Mvungi – MAELEZO, Dodoma

Kuimarika kwa Mawasiliano Kati ya Ofisi ya Rais TAMISEMI, Mikoa na Halmashauri kumetajwa kuwa chachu ya kuboreshwa kwa huduma za jamii hasa kupitia kwa mfumo mpya wa kielektroniki utakaowezesha wananchi kushiriki katika Kupanga na kuamua vipaumbele vyao katika sekta zinazogusa maisha yao  kila siku   ikiwemo Afya.

Akizungumza katika mahojiano maalum Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dkt. Asha Mahita ambaye ni mmoja wa washiriki wa mafumzo ya matumizi ya mfumo   wa kielektroniki utakaotumika  kuandaa Bajeti,Mipango na Kutoa ripoti  alisema kuwa ni chachu kwa watendaji wa Mikoa na Halmashauri zote nchini kwa kuwa wataweza kujipima na kufanya tathmini wao wenyewe kupitia mfumo huo kulingana na malengo yaliyowekwa

“Lazima sasa kila mtu afanye kazi kwa juhudi na kujituma kwa kuwa mfumo umeainisha kila jukumu na mtekelezaji wake hali itakayosaidia kuongeza uwajibikaji katika maeneo ya kutolea huduma kama Zahanati, Shule na Vituo vya Afya.” Alisisistiza Dkt. Mahita

Akifafanua Dkt. Mahita amesema kuwa mfumo huo unawawezesha watendaji kufanya uchambuzi wa Bajeti kabla ya kuiwasilisha katika ngazi husika  kwa hatua zaidi.

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe Dkt. Frank Chiduo amesema kuwa kupitia mfumo wa PlanRep  iliyoboreshwa  kutakuwa na uwazi na  uwajibikaji wa pamoja unaozingatia hali halisi ya wananchi wanaopata huduma katika vituo vya kutolea huduma.

“ Muda  uliokuwa  unatumika kuandaa  bajeti na Mipango  sasa  utapungua kwa kiasi kikubwa hivyo  kuwapa nafasi watendaji  wa Serikali kutatua changamoto  zilizojitokeza katika kuwahudumia wananchi,” alisisitiza Dkt. Chiduo.

Mradi  wa PS3 umejikita katika maeneo makuu matano ambayo ni Utawala Bora na Ushirikishwaji wananchi, Rasilimali watu, Rasilimali Fedha, Mifumo ya TEHAMA  pamoja na  Tafiti Tendaji, Tathimini na ufuatiliaji.

Mafunzo kwa watumiaji wa mfumo wa PlanRep tayari yamefanyika katika Mikoa ya Mtwara, Morogoro, Mbeya, Mwanza, Kigoma na sasa  Dodoma.Washiriki wa mafunzo hayo ni Waganga wakuu wa Mikoa, Wilaya, Wachumi, Maafisa TEHAMA, Maafisa Mipango, na Wahasibu.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi