Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Mafanikio ya TAMISEMI Miaka Mitano
Aug 28, 2020
Na Msemaji Mkuu

Na Pius Ntiga, Dodoma.

Katika kipindi cha miaka mitano cha Serikali ya Awamu ya Tano, Ofisi ya Rais-TAMISEMI imeratibu wananchi katika kuboresha miondombinu ya kutolea Huduma ya Afya kwa kujenga na kukarabati zahanati 1,198, vituo vya afya 487 na hospitali 99 katika Halmashauri ambazo hazikuwa na hospitali.

Mafanikio hayo makubwa yameelezwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- TAMISEMI, Seleman Jafo katika mahojiano maalumu na kikosi Kazi cha Amsha Amsha Dodoma cha Uhuru FM leo Jijini Dodoma wakati akiainisha mafanikio ya ofisi kwa miaka mitano.

Katika mahojiano hayo Waziri Jafo amesema katika miaka hiyo mitano akina mama wajawazito wamepata huduma ya kujifungua kwenye majengo mapya 219,764 kati ya hayo wajawazito 18,826 wakipata huduma ya upasuaji wakati wagonjwa wa kawaida waliohudumiwa na kufanyiwa upasuaji walikuwa 6,022.

Pia amesema wazee 128,108 waliohudumiwa na wagonjwa waliolazwa walikuwa 420,784 kati yao wanaume ni 176,169 na wanawake 244,615.

Aidha, matokeo ya uboreshaji miundombinu ya afya katika hospital, vituo vya afya na zahanati umenufaisha wananchi katika upatikanaji wa Huduma Bora za Afya za msingi na dharura katika mazingira rafiki na rahisi.

Kuhusu utoaji wa huduma za ustawi wa jamii amesema umeimarishwa kwa kutumia mifumo ya utoaji wa taarifa ya watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi na kuwaunganisha na huduma za msingi.

Aidha mikopo isiyo na riba yenye thamani ya shilingi 2,102,654 imetolewa kwa vikundi 582 vya watu wenye ulemavu na wazee 1,850,622 wametambuliwa.

Kati ya hao waliopatiwa ni wazee 898,753 wamepatiwa vitambulisho na wenye kadi za afya ni 684,383.

Akizungumzia kuhusu utoaji wa elimu bila malipo, amesema tangu kuanzishwa kwa Mpango huo Serikali imekwisha tumia jumla ya shilingi Trilioni 1.09, ambapo shilingi bilioni 502.2 zimetumika kwa shule za Msingi na shilingi bilioni 593.9 zimetumika kwa shule za sekondari.

Aidha licha kuongezeka kwa ufaulu katika shule za msingi na sekondari mpango huo wa elimu bure umesaidia kuongezeka idadi ya wanafunzi walioandikishwa kutoka 10,201,972 mwaka 2015 hadi kufikia 12,034,599 mwaka huu 2020.

Pia mpango huo wa elimu bure umewezesha wanafunzi wengi zaidi hasa wanotoka katika familia duni kupata fursa ya kwenda shule.

Aidha, amesema ujenzi wa shule mpya za.msingi 905 ulikuwa umekamilika hadi kufikia mwezi Juni mwaka huu 2020 na kuongeza idadi ya shule za Msingi kutoka 16,899 mwaka 2015 hadi kufikia 17,804 mwaka huu.

Kuhusu vyumba vya madarasa 17,215 vilijengwa na kuongezeka kutoka vyumba 108,504 mwaka 2016 hadi 125,719 mwaka huu sawa na ongezeko la asilimia 13.7. pia Serikali imejenga shule Mpya za sekondari 228 na hivyo kuongezeka kutoka shule 4,708 mwaka 2016 hadi 5,330 mwaka huu 2020.

Chini ya mafanikio hayo ya TAMISEMI amesema vyumba 227 vya maabara za masomo ya sayansi vimekamilishwa kwa gharama ya shilingi bilioni 2.63, ujenzi huo umeongeza idadi ya vyumba vya maabara kutoka 4,237 mwaka 2015 hadi 4,464 mwaka huu 2020.

Pia serikali imeajiri jumla ya walimu 18,181 katika shule za msingi na sekondari, kati ya walimu hao 10,666 waliajiriwa kufundisha katika shule za msingi na walimu 7,218 waliajiriwa kufundisha katika shule za sekondari.

Aidha amesema Serikali imekamilisha ukarabati wa shule kongwe za sekondari 74 kati ya shule 89 zilizopangwa kukarabatiwa ambapo ukarabati huo umegharimu shilingi bilioni 84.3.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi