Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Wenye Bima za NHIF Kulipiwa Vifaa vya Usikivu.
Jun 07, 2017
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_2894" align="aligncenter" width="750"] Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu (kulia) akimjulia hali mtoto Meckzedeck Kibona (2) aliyepandikizwa kifaa cha usikivu wakati alipozindua huduma hiyo katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili leo jijini Dar es salaam.[/caption]

 Na Jacquiline Mrisho

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu, ameuagiza Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kuhakikisha wanachama wa mfuko huo wanapata matibabu ya upandikizaji wa vifaa vya usikivu kwa kutumia kadi zao.

Waziri Ummy ametoa agizo hilo leo Jijini Dar es Saalam, alipokuwa akizindua rasmi matibabu hayo yatakayokuwa yanatolewa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili badala ya kuwapeleka wagonjwa nje ya nchi kama ilivyokuwa kipindi cha nyuma.

Waziri Ummy amesema kuwa uanzishwaji wa matibabu hayo nchini ni moja kati ya mikakati ya Serikali ya Awamu ya Tano katika kuhakikisha nchi inapunguza gharama za matibabu zilizokuwa zinatumika kwa ajili ya kuwapeleka wagonjwa kutibiwa nje ya nchi.

[caption id="attachment_2895" align="aligncenter" width="750"] Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu (kushoto) akiongea na wadau mbalimbali wa sekta ya Afya wakati wa uzinduzi wa huduma ya kupandikiza kifaa cha usikivu kwa watoto wenye matatizo ya kusikia katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili leo jijini Dar es salaam, kulia ni Mwenyekiti wa Bodi wa Muhimbili Prof.Charles Majinge.[/caption]

”Leo tunazindua rasmi matibabu haya hivyo kuanzia sasa ni mwisho kupeleka wagonjwa wa aina hii katika hospitali za nje ya nchi na ili kuhakikisha watu wengi wanapata matibabu haya wananchi wote wenye bima za NHIF watapatiwa matibabu hayo hasa kusaidiwa katika ununuzi wa kifaa husika,”alisema Mhe. Ummy.

Mhe Ummy aliongeza kuwa mbali na wagonjwa wenye bima za NHIF pia aliitaka hospitali kuzingatia Sera ya Msamaha ambapo wagonjwa wasio na uwezo wafanyiwe utaratibu wa kugharamiwa angalau gharama za kununulia vifaa hivyo.

Alisema ili kufanikisha matibabu hayo wizara italazimika kutenga bajeti ya kuwanunulia wananchi vifaa kwa lengo la kuipunguzia hospitali gharama za uendeshaji.

[caption id="attachment_2896" align="aligncenter" width="750"] Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu (kushoto) akifurahia jambo na baadhi ya watoto waliopandikizwa vifaa vya usikivu wakati wa uzinduzi wa huduma ya kupandikiza kifaa cha usikivu kwa watoto wenye matatizo ya kusikia katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili leo jijini Dar es salaam.[/caption]

Nae Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Prof. Lawrence Mseru alisema kuwa kabla ya kuanzishwa kwa matibabu hayo hospitali ilianza na uboreshaji wa miundo mbinu, ununuzi wa vifaa tiba pamoja na kuwapeleka wataalam nje ya nchi kwa ajili ya mafunzo ili kuhakikisha matibabu hayo yanatolewa kwa ubora na uhakika.

“Hospitali imetumia jumla ya shilingi bilioni 13.6 ambazo zimetumika katika kukarabati na kuongeza vyumba vya upasuaji kutoka vyumba 13 hadi kufikia vyumba 20, Kuongeza wodi za wagonjwa mahututi kutoka vitanda 21 hadi vitanda 40, kwa nyakati tofauti hospitali imepeleka wataalamu kupata mafunzo pamoja na kununua vifaa tiba,” alisema Prof.Mseru.

Prof. Mseru aliongeza kuwa nje ya nchi matibabu hayo yanagharimu kati ya shilingi milioni 80 hadi milioni 100 wakati kwa Tanzania matibabu hayo yatagharimu shilingi milioni 36 ambapo takribani shilingi milioni 31 zinatumika kununulia kifaa na kwamba matibabu yake hapa nchini ni ya  gharama ndogo ukilinganisha na nchi za nje.

[caption id="attachment_2899" align="aligncenter" width="750"] Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (kushoto) akiongea na wadau mbalimbali wa sekta ya Afya wakati wa uzinduzi wa huduma ya kupandikiza kifaa cha usikivu kwa watoto wenye matatizo ya kusikia katika Hospitali hiyo leo jijini Dar es salaam, katikati ni Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu na kulia ni Mwenyekiti wa Bodi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Prof.Charles Majinge[/caption] [caption id="attachment_2900" align="aligncenter" width="750"] Wadau mbalimbali wa sekta ya Afya na waandishi wa habari wakimsikiliza Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu hayupo pichani wakati wa uzinduzi wa huduma ya kupandikiza kifaa cha usikivu kwa watoto wenye matatizo ya kusikia katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili leo jijini Dar es salaam (Picha Na Ally Daud-WAMJW).[/caption]

Prof. Mseru alifafanua kuwa fedha hizo ni majumuisho ya mkopo wa shilingi bilioni 7.2 kutoka NHIF, shilingi milioni 600 kutoka kwa wafadhili, ruzuku kutoka Serikalini shilingi bilioni tatu na shilingi bilioni 2.8 kutoka vyanzo vya vyanzo vya mapato vya ya hospitali.

Akiwawakilisha wananchi waliowahi kupatiwa matibabu hayo na Serikali nje ya nchi, Hilda Bohela amesema kuwa kuanzishwa kwa matibabu hayo nchini ni jambo la kujivunia kwani litapunguza gharama na usumbufu ambao mgonjwa anaupata wakati akiwa katika mchakato wa kufika nchi za nje kwa ajili ya matibabu.

“Napenda kutoa rai kwa wataalam wa magonjwa haya kutoa elimu kwa wazazi ili waweze kuachana na mila potofu za kuamini kuwa mtoto akichelewa kuongea au kusikia kuwa ni tabia ya kurithi kutoka kwa ndugu zake. Pia nawashauri wazazi wenzangu kuwa makini kuwachunguza watoto wakiwa bado wadogo na kuwapeleka hospitali ili waweze kupatiwa matibabu kwa haraka,” alisema Bi. Hilda.

Matibabu hayo ndiyo ya kwanza kwa Afrika Mashariki kufanyika katika Hospitali ya Umma. Kwa mwaka huu, Hospitali ya Taifa Muhimbili imejipanga kutibu jumla ya wagonjwa 24 kwa awamu sita.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi