Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Kahama Wamshukuru Rais Magufuli kwa Kuwachangia Ujenzi wa Shule
Jan 08, 2020
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_50006" align="aligncenter" width="800"] Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Zainab Telack (Mwenye ushungi wa njano), Katibu Tawala Mkoa Bw. Albert Msovela (mwenye suti nyeusi), Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Kahama Mhe. Jasinta Mboneko na Viongozi wengine wakiwa kwenye moja ya vyumba vya madarasa ya shule ya msingi Mayila ambapo wanafunzi wa darasa la kwanza wameanza masomo yao hapo tarehe 06 Januari, 2020.[/caption]

Shule ya Msingi Mayila iliyopo Wilayani Kahama imefunguliwa rasmi huku wananchi wa wilaya hiyo wakimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Pombe Magufuli kwa kuwachangia shilingi mil. 5 ili kuhakikisha shule hiyo inakamilika.

Wazazi hao wametoa shukrani hizo mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Zainab Telack alipokwenda kukagua utekelezaji wa agizo la Mhe. Rais la kuhakikisha shule hiyo inafunguliwa mapema jana tarehe 07 Januari, 2020.

Wamesema kuwa, kukamilika kwa shule hiyo kutawapunguzia adha ya umbali wa zaidi ya kilomita 3 watoto wa kata hiyo waliokuwa wanalazimika kuvuka barabara kubwa kufuata shule kata za jirani hali iliyopelekea kuwa katika hatari ya kugongwa na magari.

“Nashukuru sana kwa shule hii, watoto wetu mwanzo walikuwa wanakwenda mbali na sisi kama wazazi tupo tayari kuendelea kushirikiana na Serikali kujenga maboma”, amesema Bw. Richard Joseph.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Nyihogo Mhe. Shadrack Mguami alikaririwa akisema kuwa “kuna wakati naamka usiku kumuombea Mhe. Rais Magufuli, sikutegemea kupata fedha kutoka kwake kwani angeweza kufanya shughuli nyingine lakini akaona atoe hapa, tunaahidi tutaendelea kumuunga mkono kwa kujenga maboma”

[caption id="attachment_50007" align="aligncenter" width="800"] Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Zainab Telack akizungumza na baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo.[/caption]

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kahama Mji Bw. Anderson Msumba amesema watoto zaidi ya 200 wameandikishwa kuanza darasa la kwanza hivyo uhitaji ni mkubwa, hata hivyo Halmashauri inaendelea kukamilisha maboma 108 na kufunga shule mpya 8.

“Tunamshukuru Mhe. Rais Magufuli ametupa mori kuhakikisha shule hii inafunguliwa” amesema Msumba.

Mhe. Rais alichangia shilingi milioni 5 ili kuongeza nguvu ya kukamilisha shule hiyo alipopita wilayani Kahama akielekea wilayani Chato mwezi Novemba, mwaka jana 2019 na kuagiza ifunguliwe mwezi Januari mwaka huu 2020.

Shule hiyo iliyokuwa na vyumba viwili vya madarasa, hivi sasa ina vyumba 8 na matundu ya vyoo 12.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi