Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Wampongeza Rais Magufuli kwa Ulinzi wa Rasilimali.
Jun 02, 2017
Na Msemaji Mkuu

Na Jonas Kamaleki

Vijana Wazalendo wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa hatua alizozichukua kuwapinga wanyonyaji wa uchumi na rasilimali za nchi kupitia sekta ya Nishati na Madini.

Pongezi hizo zimetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wazalendo Tanzania, Bwana Mwita Nyarukururu alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.

Bwana Mwita amesema ana hakika kuwa Watanzania wanafuatilia juhudi za Mhe. Rais Magufuli katika sekta ya Nishati na Madini kwa kuunda Tume ya wataalam mbalimbali kufanya uchunguzi na upembuzi yakinifu katika madini.

“Wote tumeshuhudia ripoti ya wataalam wa madini chini ya Mwenyekiti, Prof. Abdulkadir Mruma ambapo Tume imeeleza masikitiko yake makubwa dhidi ya makampuni ya madini nchini yanavyokwapua na kusafirisha raslimali zetu bila Taifa kunufaika”, alisema Mwita

Aidha, Mwita amesema kuwa unyonyaji na uhujumu uchumi katika sekta ya madini umekuwa ukipigiwa kelele kwa takriban miaka 17 na wazee pamoja na wananchi kwa ujumla juu ya tahadhari yao kwa Taifa kuwekeza katika uzalishaji wa madini kutokana na mikataba kuwa ya siri na mibovu isiyonufaisha wananchi.

Aidha wamemwomba Mhe. Rais kuvunja mikataba ambayo haina maslahi kwa taifa bila kujali udogo au ukubwa wa kampuni hizo, ikiwa ni pamoja na kupeleka Bungeni mikataba na sheria zote zinazohusu nishati na madini kwa lengo la kujadiliwa upya kwa maslahi mapana ya Taifa .

Kwa upande wake, mjumbe wa Jukwaa la Wazalendo, Bi. Rose Manumba amesema inashangaza kuona huduma za kijamii kama sekta ya Afya, Elimu na Miundombinu zinazorota kwa kukosa fedha wakati matrililioni ya fedha yanachukuliwa na wajanja wachache.

Amemuomba Mhe. Rais na wananchi kwa ujumla wasichoke katika mapambano haya ya kukomesha wizi wa raslimali za Watanzania walizopewa na Mungu.

“Kwa kweli tumuunge mkono Mheshimiwa Rais katika vita hii ili nchi yetu na raslimali zake ziwe na manufaa kwa kizazi chetu na vizazi vijavyo”, alisema Manumba.

Mwezi uliopita Mhe. Rais alipokea Ripoti ya uchunguzi wa Makinikila ambayo ilionyesha kuwa tani za dhahabu na madini mengine yenye thamani kubwa yalipatikana kwenye mchanga uliokuwa usafirishwe nje ya nchi. Katika ripoti hiyo jumla ya takriban tani 15 za madini zilikutwa kwenye makontena 277 ya makinikila yayozuiliwa kusafirishwa nje na Mhe. Rais Magufuli, thamani yake inakadiriwa kuwa ni shilingi za Kitanzania trililioni 1.3.

Kufuatia ripoti hiyo, uteuzi wa Waziri mwenye dhamna ya Nishati na Madini, Prof. Sospiter Muhongo ulitenguliwa na Mhe. Rais, na aliyekuwa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Madini Nchini, alisimamishwa kazi.

Juhudi hizi za Mhe. Rais katika kupambana na ufisadi nchini zimeungwa mkono na watanzania wengi wakiwemo viongozi wa dini.

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi