Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Wakimbizi Zaidi Raia wa Burundi Kurejea Nyumbani Wiki Hii
Sep 10, 2017
Na Msemaji Mkuu

Na: Mwandishi Wetu

Makundi mawili kila moja likiwa na wastani wa wakimbizi 350 raia wa Burundi kati ya wakimbizi 13,000 ambao hadi tarehe 07 Septemba, 2017 walikuwa wamejiorodhesha kwa hiari kurejea nyumbani yanatarajiwa kuondoka nchini wiki hii.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Wakimbizi, katika Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Deusdedit Masusu, misafara saba yenye wastani wa wakimbizi 350 inatarajiwa kuondoka nchini kurejea Burundi katika mwezi huu wa Septemba, 2017 miwili kati ya hiyo ikiondoka siku ya Jumanne tarehe 12 na Alhamisi tarehe 14 Septemba, 2017.

Bwana Masusu aliieleza Idara ya Habari- MAELEZO ofisini kwake hivi karibuni kuwa idadi ya wakimbizi wataorejeshwa nyumbani inatarajiwa kuongezeka kadri zoezi hilo ambalo lilianza Alhamisi wiki iliyopita litakavyoshika kasi.

“Mpango wetu unaonesha kuwa kwa mwezi huu wa Septemba wakimbizi waliondoka tarehe 7 na wengine wataondoka tarehe 12, 14, 19, 21, 26 na 28 kwa watani wa wakimbizi 350”alisema lakini hata hivyo alieleza kuwa kundi la kwanza lililoondoka lilikuwa na wakimbizi 301 tu.

Mkurugenzi Msaidizi huyo alieleza kuwa kasi ya kujiandikisha kwa hiari kwa wakimbizi hao raia wa Burundi inatarajiwa kuongezeka zaidi kufuatia makundi hayo kurejea nyumbani kwa kuwa mafanikio ya zoezi hilo yatakuwa kichocheo kwa wengine kutaka kurejea nyumbani.

“Tunatarajia ikifika mwishoni mwa mwezi huu kasi ya kujiorodhesha itaongezeka sana kwa kuwa watakaorejea watatoa taarifa zaidi kwa wenzao hivyo kwa wale wanaosita bila ya shaka wengi wao hawataona sababu ya kuendelea kubaki makambini” Alisema bwana Masusu.

Alibanisha kuwa urahisi wa mawasiliano utawezesha wakimnizi waliorejea kuwapa wenzao mrejesho wa hali ilivyo nchini kwao na hivyo kutoa hamasa kwa walioko makambini nao kutaka kurejea nyumbani.

Mkurugenzi Msaidizi huyo aliongeza kuwa kinachofanyika ni kuhakikisha zoezi hilo linafanyika kwa umakini mkubwa na kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa ili wakimbizi hao waweze kurejea nyumbani kwa usalama na heshima.

“Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) ndilo linalotoa usafiri wa wakimbizi na mzigo yao kutoka makambini hadi nchini Burundi na wakimbizi wanaorejea wanasaidiwa chakula kupitia Shirika la Mapngo wa Chakula (WFP) kwa miezi mitatu” Alifafanua bwana Masusu.

Zoezi la kuwarejesha wakimbizi hao wa Burundi linafanyika kufuatia makubaliano yaliyofikiwa tarehe 31 Agosti, 2017 jijini Dar Es Salaam kati ya Serikali za Tanzania, Burundi na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia wakimbizi (UNHCR).

Zoezi la kuwarejesha wakimbizi kundi la kwanza, kwa upande wa Tanzania, lilishuhudiwa na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Brigedia Jenerali (Mstaafu ) Emmanual Maganga, Kamati ya Ulinzi na Usalama  wa Mkoa Kogoma pamoja Mwakilishi wa UNHCR nchini na maafisa wengine wa Wizara ya Mambo ya Ndani.

Msafara wa Burundi uliongozwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani wa Nchi hiyo Theranse Ndayiragije, Mwakilishi kutoka Ofisi ya UNHCR Burundi na washiriki wengine. Tukio hilo lilishuhudiwa pia na Ofisa Ubalozi wa Tanzania nchini Burundi.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi