Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Wagonjwa 300 Wafanyiwa Uchunguzi wa Macho Wilayani Muheza
Jul 18, 2018
Na Msemaji Mkuu

MKUU wa wilaya ya Muheza Mhandisi Mwanasha Tumbo akizungumza na wananchi wa wilaya hiyo waliofanyiwa uchunguzi wa  matatizo ya macho  wakati wa zoezi la kufunga kambi ya matibabu ya tiba ya macho iliyoendeshwa na Taasisi ya isiyokuwa ya kiserikali ya Medewell Health Centre kwenye kituo cha Afya cha Ubwari wilayani Muheza

Zaidi ya wagonjwa 300 wamefanyiwa uchunguzi wa matatizo ya macho wilayani Muheza mkoani Tanga kwenye zoezi lililoendeshwa na wataalam kutoka Hospitali ya Medewell iliyopo wilaya ya Kibaha mkoani Pwani huku 121 wakibainika kuwa na tatizo la mtoto wa jicho.

Hayo yalibainishwa na Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya Muheza, Julius Mgeni wakati wa zoezi la kufunga kambi ya matibabu ya tiba ya macho iliyoendeshwa na Taasisi isiyokuwa ya kiserikali ya Medewell Health Centre kwenye kituo cha Afya cha Ubwari wilayani Muheza

Alisema wataalam hao wamekuwa wakiendesha zoezi hilo mara kwa mara ambalo limekuwa na mafanikio makubwa kwa wagonjwa kupona na kuweza kuona na hivyo kupunguza idadi ya watu wenye changamoto za namna hiyo.

Alisema baada ya wagonjwa hao kufanyiwa uchunguzi, jumla ya wagonjwa 121 walibainika kuwa na tatizo la mtoto wa jicho ambao waliweza kufanyiwa upasuaji na kupewa dawa ambazo wanapaswa kuzitumia wakati wa matibabu hayo huku watu 191 wakipatiwa matibabu ya kawaida.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Medewell Munir Meral akizungumza katika ufungaji wa kambi hiyo kushoto ni Mkuu wa wilaya ya Muheza Mhandisi Mwanasha Tumbo

Awali, Mkuu wa Wilaya ya Muheza Mhandisi Mwanasha Tumbo alisema zoezi la uchunguzi na operesheni ambazo zimekuwa zikifanyika vimekuwa na mafanikio makubwa jambo ambalo limeongeza mwamko wa wananchi kutoka maeneo mbalimbali ambao wanajitokeza kila wakati.

“Kwa kweli niwapongeze Medewell kwa kuendesha matibabu haya ya mtoto wa Jicho na ya kawaida kwani yamekuwa faraja kubwa sana na faida yake imeweza kuonekana na kuwasaidia watu  kuweza kurudi kwenye hali zao za kawaida”Alisema.

Alisema matibabu hayo yatawawezesha watu kuweza kuona jambo ambalo litawasaidia wananchi wengi waliokumbwa na tatizo hilo kuweza kufanya shughuli za uzalishaji mali ikiwemo zile za kujiingizia kipato na hivyo kusaidia kuinua uchumi wao na jamii zinazowazunguka.

Sehemu ya wananchi kutoka maeneo mbalimbali mkoani Tanga waliopatiwa matibabu ya macho

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya Medewell Munir Meral alisema wananchi wamefarijika kwa kiasi kikubwa kutokana na baadhi yao kukata tamaa kutokana na uwepo wa matatizo hayo ambayo kiuhalisia yana gharama kukabiliana nayo.

Alisema mbali  na kutoa msaada wa matibabu bure pia kwa kushirikiana na Betacharitable Trust toka Uingereza wamekabidhi kifaa cha kupima na kuchunhuza matatizo ya macho (slit lamp) yenye thamani ya zaidi ya Shilingi Milioni kumi na vifaa vya kupimia miwani (tria set).

Alisema utolewaji wa vifaa hivyo utarahisisha kituo hicho cha afya kuweza kuanza kufanya uchunguzi wa matatizo ya macho kupitia wataalam waliopo jambo ambalo lilikuwa likishindikana kufanyika kutokana na uhaba wa vifaa hivyo tiba.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi