Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Utoroshaji wa Madini Chunya sasa basi
Dec 03, 2019
Na Msemaji Mkuu

Nuru Mwasampeta na Greyson Mwase, Chunya
Desemba 03, 2019
Katika kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Wizara ya Madini kwenye udhibiti wa utoroshwaji wa madini kupitia masoko ya madini yaliyoanzishwa nchini, wachimbaji wa madini Wilayani Chunya wameazimia kutumia Soko la Madini Chunya na kutokutorosha madini.
Akizungumza kwa niaba ya wachimbaji wa madini katika eneo la Soweto Wilayani Chunya Mkoani Mbeya kupitia  mahojiano kwenye maandalizi ya kipindi maalum chenye kuelezea mafaniko  ya Sekta ya Madini, Mmiliki wa Kampuni ya Uchimbaji wa Madini ya Mdimi Investment C. Limited, Mdimi Msigwa leo tarehe 03 Desemba, 2019 alieleza kuwa, Serikali imeweka mazingira rafiki na salama kwa wafanyabiashara na wachimbaji wa madini kwa kuwaanzishia masoko ya madini, hivyo hakuna haja ya kutorosha madini.
Akielezea mafanikio ya mgodi wake tangu kuanzishwa kwa Soko la Madini la Chunya, Msigwa alieleza kuwa, kabla ya kuanzishwa kwa soko hilo alikuwa na uwezo wa kuajiri wafanyakazi wachache kutokana na dhahabu yake kutokuwa na soko la uhakika na kuongeza kuwa baada ya uanzishwaji wa soko aliweza kuongeza ajira kutokana na biashara ya madini ya dhahabu kuwa ya uhakika.
Katika hatua nyingine, mchimbaji mwingine wa dhahabu katika eneo la Chokaa, Wilayani Chunya, Ahobokile Mwasyeba mbali na kupongeza juhudi zinazofanywa na Wizara ya Madini kupitia Tume ya Madini alieleza manufaa ya soko hilo kuwa ni pamoja upatikanaji wa wanunuzi wa uhakika wa madini hayo na bei elekezi inayotolewa na Serikali
 "Tulikuwa tunasafiri kwa muda mrefu kwenda kuuza madini kwa wahindi jijini Dar es Salaam lakini sasa tunauzia madini yetu hapa hapa Chunya tena kwa bei elekezi" alisema Mwasyeba
Alifafanua kuwa uwepo wa soko umeongeza mwamko wa wananchi wa Chunya kufanya kazi kwenye machimbo kutokana na kipato cha uhakika kwa wamiliki wa migodi mara baada ya kuuza madini kwenye soko la madini.
Akielezea namna soko lilivyowasaidia kwenye eneo la bei elekezi, Ahombwile alieleza kuwa tangu kuanzishwa kwa soko la madini bei ya gramu moja ya dhahabu haijawahi kupungua  chini ya  90,000 tofauti na awali ambapo walikuwa wanauza kwa bei ya hasara.
Naye Meneja ya Benki ya CRDB Chunya, Hamis Mbinga akielezea mabadiliko ya soko kwenye mzunguko wa fedha  alisema kuwa  wafanyabiashara wa madini wameanza kutumia benki hiyo kutunza fedha zao hivyo kuondokana na adha ya kuvamiwa na majambazi.
Aliongeza kuwa Benki ya CRDB imeanza kuweka mikakati ya kuwasaidia wafanyabiashara wa madini kwa kuwapatia mikopo kutokana na uwepo wa taarifa zao za fedha kwenye benki hiyo.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi