Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

TMS Kutoa Ajira Zaidi ya 6000 Nchini
Dec 05, 2017
Na Msemaji Mkuu

Jonas Kamaleki.

TMS Consultants Ltd imejiandaa kutoa ajira 6000 nchini katika juhudi za ujenzi wa viwanda na kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana.

Hayo yameelezwa leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya TMS Consultants Ltd, Sebatian Kingu alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.

Akifafanua kuhusu ajira hizo, Kingu amesema kuwa kampuni yake itajenga mtandao wa matawi 6,000 nchi nzima ya Tanzania hivyo kufikisha huduma zake hadi vijijini badala ya kuishia mijini.

 "Kwa kutumia mtandao wa matawi yetu ya mtindo wa Franchasing, TMS kwa makubaliano  ya kimkataba na taasisi ka za Mifuko ya Hifadhi za jamii kama vile NSSF, PPF, PSPF, LAPF, tutaweza kuzifikisha huduma huduma hadi vijijini ambapo wao hawana ofisi lakini wana huduma za wakulima, wavuvi, wafugaji na wajasiriamali wengine wadogo wadogo", alisema Kingu

Kingu amesema matawi hayo yatamilikiwa na wananchi wenyewe ambao watakuwa wanatoa faida kwa TMS.

Bwana Kingu amesema kuwa ipo mitaji ya kutosha kwa wale wanotaka kuwekeza katika viwanda  vidogo, vya kati na vikubwa na kwamba kinachohitajika ni kuingia ubia na wenye mitaji.

"Tunashirikiana na kampuni 10,000 Duniani ambazo ziko tayari kutoa mitaji kwa njia ya ubia na watanzania, hivyo hatuna shaka na fedha za mtaji", alisema Kingu.

Amewashauri wananchi watumie hiyo fursa ili azima ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kujenga uchumi wa viwanda iweze kutimia.

Aidha Kingu amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa jitihada zake za kukuza uchumi kwa kupitia utekelezaji wa miradi mikubwa ikiwemo ya ujenzi wa reli ya kisasa (Standard Gauge), kufufua Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) ambalo sasa linazo ndege tatu na utekelezaji wa mradi mkubwa wa umeme wa Steglers Gorge ambao utazalisha megawatt 2100 na kuondoa tatizo la umeme nchini.

Pia Rais amepongezwa kwa vita yake ya uchumi hasa kupambana na ufisadi, kulinda rasilimali za taifa ikiwemo madini na maliasili nyinginezo na kurudisha nidhamu katika utumishi wa umma.

Amewataka watanzania kumuunga mkono Rais Magufuli kwa kuwekeza katika viwanda ambavyo vitatumia rasilimali za humu nchini na hivyo kupanua wigo wa ajira.

Kingu amesema kuwa zipo huduma mpya za Bima amabazo zimewalenga wakulima na wafugaji ambao wanafanya shughuli za kibiashara lakini haziwafikii.

Ameongeza kuwa huu ni wakati muafaka kwa mfumo uliojengwa kwa kipindi kirefu, takriban miaka 25 kuwezesha upatikanaji wa huduma hizo kuwa endelevu badala ya kumtegemea mwanzilishi, hivyo mfumo wa matawi hayo utakuwa na uwezo wa kujiendesha wenyewe.

Katika Mpango wa Maendelo ya miaka mitano wa 2016/17-2020/21 inakadiriwa kuwa Miradi ya Maendeleo ya Serikali itahitaji kiasi cha TZS. trililioni 107. Kati ya hizo TZS trililioni 59 ambazo ni 55% zinategemewa zitokane na vyanzo vya Serikali na trililioni 48 sawa na 45% zinategemewa zitokane na Sekta binafsi kwa mtindo wa ubia kati ya Serikali na Sekta binafsi (PPP)

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi