Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

TAPSEA Mkoa wa Dodoma Wasaidia Waathirika wa Hanang
Dec 29, 2023
TAPSEA Mkoa wa Dodoma Wasaidia Waathirika wa Hanang
Chama cha Waandishi Waendesha Ofisi (TAPSEA), Mkoa wa Dodoma wakitoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa waathirika wa maporomoko ya tope yaliyotokea wilayani Hanang mkoani Manyara.
Na Mwandishi wa Umma

Chama cha Waandishi Waendesha Ofisi (TAPSEA), Mkoa wa Dodoma kimetoa pole na msaada wa vifaa mbalimbali kwa waathirika wa maporomoko ya tope yaliyotokea wilayani Hanang mkoani Manyara.

Msaada huo ambao ni mchango wa TAPSEA mkoa wa Dodoma ni pamoja na vifaa vya shule yakiwemo madaftari, sare za shule, kalamu na nguo vyote vikiwa na jumla ya takribani shilingi milioni 5.

Mwakilishi wa Chama hicho, Bi, Conjeta Chambila amesema chama chao kimeona umuhimu wa kuchangiana kwa lengo la kuweza kuwasaidia wenzao.

Pia Bi Chambila, amemshukuru Katibu Mkuu, Wizara ya Ujenzi Balozi, Mhandisi Aisha Amour kwa kuweza kuwawezesha usafiri wa kutoka Dodoma hadi kufika mkoani Manyara.

“Tunamshukuru sana Katibu Mkuu wa Ujenzi, kwa kuweza kutukusanya pamoja na kutuwezesha kutupa usafiri, ikiwa tunatoka ofisi mbalimbali” amesema Chambila.

Aidha, Chama hicho kimetoa wito kwa Waandishi Waendesha Ofisi wengine wa mikoa ya karibu kuweza kuwasaidia waathirika hao ambao wamepoteza vitu vyao wakati wa maafa hayo.

Kwa upande wake, Katibu Tawala (DAS), Mkoa wa Manyara, Bw. Athuman Likeyekeye amewashukuru Waandishi Waendesha Ofisi kutoka mkoa wa Dodoma kwa upendo wao wa kuja kuwasaidia waathirika hao katika kipindi hiki cha Sikukuu za Mwaka mpya.

Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na uratibu, kwa kushirikiana na ofisi za Wakuu wa Mikoa na Wilaya, wanaendelea kupokea misaada mbalimbali kwa ajili ya waathirika wa maporomoko ya tope, mkoani Manyara.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi