Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

TACAIDS Yajidhatiti Kuzuia Maambukizi Mapya ya VVU
Aug 30, 2019
Na Msemaji Mkuu

 

Na; Mwandishi Wetu

Tume ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI (TACAIDS) imejidhatiti kukabiliana na maambukizi mapya ya ugonjwa huo kwa kuanzisha vituo vya kutoa huduma za ushauri nasaha na upimaji katika maeneo yote ya barabara kuu za kwenda nchi jirani.

Akizungumza katika kipindi cha “TUNATEKELEAZA” Mkurugenzi Mtendaji wa Tume hiyo Dkt. Leonard Maboko amesema mpaka sasa vituo 20 vimeanza kutoa huduma katika barabara kuu za kuelekea nchi jirani ili kuyafikia makundi maalum kama madereva na vijana wanaoishi katika maeneo ambayo yana mikusanyiko mikubwa ya watu kutokana na shughuli za kibiashara.

“Katika mradi huu bilioni 12 zimetumika katika kuanzisha vituo hivyo 20 ambapo matarajio yetu katika mwaka 2019/20 tutaanzisha vituo vingine 20 kwa lengo la kuhakikisha tunayafikia makundi maalum kama wavuvi, vijana  wa kiume na kike” alisisitiza Dkt.  Maboko

Akifafanua Dkt. Maboko amesema kuwa Tume hiyo itaendelea kuchukua jitihada za makusudi katika kuzuia maambukuzi mapya na kuhakikisha wale walioathirika wanapatiwa dawa za kufubaza virusi vya ugonjwa huo kwa wakati.

Aliongeza kuwa, baadhi ya maeneo yanawekewa mkakati maalum kutokana na kuongezeka kwa kiwango cha maambukizi ikiwemo mkoa wa Dodoma na kuwataka wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi ya ugonjwa huo kwa kuepuka ngono zembe.

Aidha, Dkt Maboko aliwataka vijana kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi kwa kuzingatia kanuni zitakazowaepusha na maambukizi mapya kwa kuwa wanategemewa kama nguvu kazi ya Taifa.

Tume ya Kudhibiti UKIMWI imekuwa ikitekeleza mikakati mbalimbali yakukabiliana na ugonjwa huo ikiwemo kutoa elimu kwa umma na makundi maalum yaliyo katika hatari ya kupata maambukizi ya ugonjwa wa UKIMWI.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi