Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Taarifa kwa Umma
Jun 03, 2020
Na Msemaji Mkuu

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 03 Juni, 2020 amekutana na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein katika kikao cha ndani kilichofanyika Ikulu, Chamwino Mkoani Dodoma.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Makamu Mwenyekiti CCM Bara Ndg. Philip Mangula na Katibu Mkuu wa CCM Ndg. Bashiru Ally Kakurwa ambapo viongozi hao wamezungumzia masuala ya CCM.

Baada ya kikao hicho, Mhe. Rais Shein amekwenda kuweka udongo katika jiwe la msingi la ujenzi wa Ofisi za Ikulu na kukagua maendeleo ya kazi ya ujenzi wa ofisi hizo inayofanywa na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kupitia shirika lake la Suma JKT.

Mhe. Rais Shein amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa kumpa fursa ya kwenda kuweka udongo ikiwa ni kumbukumbu ya ujenzi wa ofisi hizo na amebainisha kuwa kujengwa kwa ofisi hiyo ni heshima kwa Taifa na tafsiri sahihi ya kujitawala.

“Huko ndio kujitawala, kutawaliwa sio kuzuri, mtawala anafanya anavyotaka yeye, anafanya kwa utashi wake pale anapotaka yeye kufanya, tunapochukua hatua ya kujitawala wenyewe tunafanya mambo makubwa kama haya kwa ajili ya wananchi, hii ofisi ni ya wananchi wa Tanzania” amesema Mhe. Rais Shein.

Mhe. Rais Shein amewasalimu vijana wa JKT wanaofanya kazi za ujenzi wa ofisi hizo, amewapongeza kwa kazi nzuri wanayoifanya na amewataka kujivunia fursa hiyo adhimu ya kujenga ofisi ya Ikulu za nchi yao, badala ya kazi hiyo kufanywa na kampuni za nje ya nchi kama ambavyo hufanyika katika maeneo mengi.

Gerson Msigwa Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU Chamwino 03 Juni, 2020

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi