Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Serikali Kupima Maeneo Yote Mwaka Huu Kuepusha Migogoro
Jan 28, 2018
Na Msemaji Mkuu

Na. Hassan Mabuye.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mheshimiwa William Lukuvi amezitaka Wizara, Taasisi za Serikali na Vyombo vyote vya Umma kupima maeneo yao na kuyawekea alama za mipaka ili kuepusha maeneo hayo kuvamiwa na wananchi..

Waziri Lukuvi amesema hayo mara baada ya kukagua maeneo yaliyo na migogoro ya ardhi katika Manispaa ya Ilemela mkoani Mwanza.

Aidha, Mheshimiwa Lukuvi akiambata na Naibu wake, Angelina Mabula ambaye ni mbunge wa Jimbo la Ilemela mkoani Mwanza walitembelea maeneo yaliyovamiwa na wananchi ya Polisi Kigoto-Kirumba lililovamiwa na wananchi, Uwanja wa Ndege wa Mwanza na eneo la Jeshi la Wananchi wa Tanzania la Nyamirolerwa katika manispaa ya Ilemela mkoani Mwanza.

Kutokana na kujionea uvamizi huo wa maeneo hayo, Waziri Lukuvi amezitaka taazizi zote za Serikali kupima maeneo yao ili wananchi waweze kutambua maeneo ya Serikali na wasiweze kuyavamia jambo ambalo huzaa migogoro.

Hata hivyo Waziri Lukuvi amewataka wananchi waliojenga ndani ya hifadhi ya Uwanja wa Ndege wa Mwanza kuondoa maendelezo yao ndani ya siku saba kabla ya kuchukuliwa hatua kwakuwa ni wavamizi na hawaruhusiwi kukaa karibu na eneo linalorusha na kutua vyombo vya anga jambo ambalo ni hatari kwao na usalama wa vyombo hivyo.

"Hawa waliojenga ni wavamizi na watambue hivyo majibu tutatoa badaye nini tutafanya lakini wajue maisha yao siyo ya hapo ndani ya uwanja," alisema Lukuvi.

Katika hatua nyingine Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi amezitaka Halmashauri zote nchini kukamilisha zoezi la ukusanyaji wa kodi ya Ardhi kabla ya tarehe 30 mwezi Aprili mwaka huu.

Aliyasema hayo baada ya kukutana na watumishi na wakuu wa idara wa Manispaa ya Ilemela na wa jiji la Mwanza wakati wa ziara ya kukagua mifumo ya ulipaji kodi ya pango la ardhi na maendeleo ya zoezi la urasimishaji makazi mkoani Mwanza.

"Kazi ya ulipaji kodi sio jambo la hiari ni lazima, kila Mkurugenzi katika wilaya yake ifikapo Aprili 30, mwaka huu awe amesha kusanya kodi na baada ya hapo watakaoshindwa kutekeleza nitatangaza majina yao katika magazeti ya umma na wataenda kulipia mahakamani, ili malengo yetu yatimie,"  amesema Lukuvi

Aidha Lukuvi amezitaka halmashauri zote kupima viwanja vyote na kuwaagiza maafisa ardhi kutoa hati kwa wananchi kulingana na majina yao halisia kama yalivyo katika vitambulisho vya taifa vilivyosajiliwa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) ili kuepusha usumbufu wakati wa uingizwaji katika mfumo.

Awali akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa zoezi la urasimishaji makazi na makusanyo ya kodi ya pango la Ardhi, Mkuu wa Idara ya mipango miji na ardhi Manispaa ya Ilemela, Shukrani Kyando, alisema miongoni mwa changamoto zinazowakabili ni wananchi kuvamia maeneo yaliyopimwa na kutengewa Kwa ajili ya matumizi ya umma .

"Kwa mwaka huu wa fedha hadi kufikia sasa tumekusanya Sh bilioni 1.8 sawa na asilimia 72 ya lengo la makusanyo ya Sh bilioni 2.5, na jumla ya hati 5,277 Kati ya hati 16,141 zimeandaliwa katika maeneo yaliyorasimishwa Huku jumla ya viwanja 35,336 tayari vimeingizwa katika mfumo, " alisema.

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi