Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Serikali Imepata Ufadhili wa Bil. 66 kwa Ajili ya Maboresho ya Vituo vya Afya
Sep 13, 2017
Na Msemaji Mkuu

Na: Lilian Lundo – MAELEZO – Dodoma.

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imepata ufadhili wa Shilingi Bilioni 66 kutoka Benki ya Dunia kwa ajili ya kuboresha vituo vya Afya nchini.

Naibu Waziri wa Wizara hiyo Dkt. Hamisi Kigwangala amesema hayo leo Mjini Dodoma allipokuwa akijibu swali la Mbunge wa viti maalum Mhe. Khadija Nassir Ali juu ya utekelezaji wa agizo la Mwandoya la kuanzisha huduma za upasuaji katika vituo vyote vya Afya nchini.

“Wizara imeshirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI kubainisha vituo 100 vitakavyoboreshwa ili kutoa huduma za dharura za upasuaji wa kutoa mtoto tumboni,” alisema Dkt. Kigwangala.

Aidha amesema kuwa, fedha za utekelezaji wamaboresho ya vituo hivyo zimeanza kupelekwa katika halmashauri husika ili kuanza maboresho katika vituo hivyo.

“Agizo la Mwandoya linazitaka  Halmashauri  nchini  kutumia fedha zao za ndani kuhakikisha zimejenga au kukarabati vyumba vya upasuaji kwa kipindi cha miezi Sita ili kupunguza vifo vya mama na mtoto na kupeleka huduma karibu na wananchi,” alifafanua Dkt. Kigwangala.

Ameendelea kwa kusema kuwa baada ya muda huo kumalizika, Wizara iliongeza miezi mitatu ili kukamilisha agizo hilo. Aidha wataalam wa Wizara hiyo kwa sasa wanatembelea vituo katika Halmashauri nchi nzima kwa ajili ya kufanya tathmini, kubaini waliotekeleza na ambao hawajatekeleza ili hatua za kinidhamu zifuate.

Wizara hiyo hadi sasa imesambaza vifungashio (delivery packs) 60,000 kwa mikoa sita (6) ya Kanda ya Ziwa ambayo vifo vingi vya mama wajawazito  na watoto vimekuwa vikitokea huko. Aidha ni jukumu la kila Halmashauri kuweka mahitaji ya vifungashio kwenye mpango kabambe wa Afya wa halmashauri (Comprehensive Council Health Plan) (CCHP).

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi