Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

RC Makonda: Kinondoni ni Mfano wa Kuigwa kwa Utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo
Jun 30, 2020
Na Msemaji Mkuu

Na Mwandishi Wetu

Halmashauri za Mkoa wa Dar es salaam zimetakiwa kuiga mfano wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa kutumia vyanzo vya mapato ya ndani, Serikali Kuu pamoja na wadau kama ilivyotekelezwa katika Manispaa ya Kinondoni.

Kauli hiyo imetolewa leo na Mkuu wa Mkoa wa Dar Es Salaam, Paul Makonda wakati akihitimisha ziara yake ya siku mbili kwa jimbo la Kinondoni na Kawe yenye lengo la kukabidhi miradi  kwa kamati ya siasa ya Mkoa.

Amesema kuwa kila Halmashauri katika Mkoa wa Dar es Salaam inakusanya mapato hivyo zinapaswa kutekeleza miradi ambayo itaaacha alama kama ambavyo Manispaa ya Kinondoni imeweka alama katika miradi mikubwa ya maendeleo chini ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Rais Dkt. John Pombe  Magufuli pamoja na usimamizi mzuri wa Mkurugenzi mzalendo Ndg. Aron Kagurumjuli.

"Kinondoni nawapongeza sana, mmefanya kazi inayoonekana nakuacha alama kwa Wananchi, kipindi cha nyuma haya mambo hayakuwepo licha ya kwamba Manispaa zilikuwa zinakusanya mapato lakini katika uongozi wa miaka mitano ya Dkt. Magufuli mmeitendea haki ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), " amesema Makonda.

Akizungumzia mradi wa soko la kisasa la Magomeni, Makonda  amesema  soko hilo lililojengwa kwa fedha kutoka Serikali Kuu, ni  chanzo kikubwa cha mapato katika Manispaa ya Kinondoni  litakaloongeza hadhi ya wafanyabishara watakaoendesha shuguli zao bila kubugudhiwa.

Awali akimkaribisha Mkuu wa Mkoa,  Chongolo amesema kuwa katika Wilaya hiyo Mkurugenzi pamoja na timu yake wamefanikiwa kukamilisha miradi kwa wakati na kwamba wanapoikabidhi kwa kamati hiyo inatoa fursa kuendelea kutekeleza miradi mingine.

Chongolo amesema kuwa miradi iliyotembelewa Jimbo la Kawe na Kinondoni ilikuwa ni alama ya kukabidhi miradi hiyo kwa CCM ngazi ya mkoa ikiwa ni baada ya ukamilishwaji wake na kueleza kuwa soko la kisasa la Magomeni hadi sasa limekamilika kwa asilimia 95 na kwamba hadi kufikia Agosti mwaka huu litakuwa limeanza kutumika na wafanyabiashara.

 Katika ziara hiyo Mkuu wa Mkoa Makonda ametembelea miradi mbalimbali ambayo ni ujenzi wa Hospital ya Wilaya iliyopo Mabwepande, Kiwanda Cha kuchakata taka, Shule ya wasichana Mabwe Tumaini na Zahanati ya Bunju.

Miradi mingine ni ujenzi wa matanki ya maji , ujenzi wa barabara ya njia nne kutoka Shekilango hadi Bamaga, Soko la Kisasa Magomeni, Kituo cha Afya kigogo, Zahanati ya Mikoroshini, Uwanja wa kisasa wa mpira wa miguu mwenge pamoja na Stendi ya daladala iliyopo Mwenge.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi