Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Rais Magufuli Afungua Kiwanda cha Sayona Mwanza
Oct 30, 2017
Na Msemaji Mkuu

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

KURUGENZI YA MAWASILIANO YA RAIS IKULU

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amefungua kiwanda cha vinywaji baridi cha Sayona kilichopo Nyakato Mjini Mwanza kilichojengwa na kampuni ya Kitanzania ya Motisan kwa gharama ya takribani Shilingi Bilioni 11 na Milioni 800.TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Kiwanda hiki cha kisasa ambacho kimejengwa kwa muda wa mwaka mmoja na nusu kina uwezo wa kuzalisha chupa 1,200 kwa dakika moja katika mitambo yake minne ya kuzalisha vinywaji baridi pamoja na chupa 100 za maji, kimezalisha ajira za watu 200 na kinaungana na kiwanda kingine cha vinywaji baridi cha Sayona kilichopo Mboga Mkoani Pwani kusindika matunda ya wakulima na kuinua hali zao za maisha.

Akizungumza baada ya Mhe. Rais kufungua kiwanda cha Sayona Mwanza, Mkurugenzi Mkuu wa Motisan Group Bw. Subhash Patel amesema kampuni yake imedhamiria kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano za kujikita katika uchumi wa viwanda na ameahidi kuwa mwaka ujao wa 2018 kampuni hiyo itajenga viwanda vingine vitano.

Mhe. Rais Magufuli amempongeza Bw. Subhash Patel kwa uwekezaji mkubwa anaoufanya katika viwanda na amemtaka yeye pamoja na wafanyabiashara wengine kutumia muda huu kuwekeza zaidi katika viwanda na kwamba Serikali yake itawaunga mkono.

“Bw. Subhash nakupongeza sana, wewe jenga viwanda Serikali itakuunga mkono, na nataka niwaambie wafanyabiashara na wawekezaji, huu ndio wakati wa kuwekeza na mimi nawapenda wafanyabiashara na wawekezaji, hapa kusingekuwa na kiwanda hiki, vijana hawa 200 wasingepata ajira, nataka kukupongeza sana hata kwa mpango wako wa kujenga viwanda vingine vitano mwakani, hii ni safi sana” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Mhe. Dkt. Magufuli amempongeza Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Bw. John Mongella kwa juhudi anazofanya kusimamia utekelezaji wa sera ya viwanda kwa kuhakikisha viwanda vinaanzishwa na ametaka juhudi hizo ziendelee ili Mwanza irejeshe historia yake ya kuwa na viwanda vingi vinavyozalisha ajira na kukuza uchumi wa mkoa.

Wakizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika eneo la Nyakato Mwatex Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe. Charles Mwijage, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa Mnyaa na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Anjelina Mabula wamewahakikishia wananchi wa Mwanza kuwa Serikali ya Awamu ya Tano inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuuendeleza Mkoa wa Mwanza kwa kuhakikisha viwanda zaidi vinajengwa, miundombinu inaimarishwa na migogoro ya ardhi inamalizwa na wamewataka wananchi wajielekeze zaidi katika uzalishaji mali.

Katika mkutano huo, Mbunge wa Nyamagana Mhe. Stanslaus Mabula, Umoja wa Wamachinga na Umoja wa Wanawake wajasiriamali Mkoa wa Mwanza wamemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa juhudi kubwa anazofanya kuwajali wananchi hasa wa hali ya chini na kupigania maendeleo ya Taifa zima.

Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli amezungumzia utekelezaji wa ahadi ya kutoa Shilingi Milioni 50 kwa kila Kijiji ama Mtaa kwa kueleza kuwa Serikali imeona njia bora ni kuelekeza fedha hizo katika miradi mikubwa yenye manufaa na matokeo mapana kwa wananchi na amesisitiza kuwa utekelezaji wa dhamira hiyo umeanza.

Amebainisha kuwa pamoja na hatua hizo Serikali inaendelea kukabiliana na wote waliojihusisha na ufisadi wa mali za umma na kwamba haitasita kuchukua hatua za kisheria hata kama wahusika watakimbia, kujificha ama kutetewa mahali popote.

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Mwanza

30 Oktoba, 2017

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi