Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Pinda Awafunda Watendaji wa Sekta ya Ardhi Mwanza
Jan 29, 2024
Pinda Awafunda Watendaji wa Sekta ya Ardhi Mwanza
Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Gephrey Pinda akisisitiza jambo wakati akizungumza na wakuu wa idara na vitengo wanaosimamia sekta ya ardhi katika Halmashauri ya Jiji la Mwanza pamoja na wale wa Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Mwanza akiwa katika ziara yake mkoani humo tarehe 29 Januari, 2024.
Na Munir Shemweta, WANMM MWANZA

Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Geophrey Pinda amewafunda watendaji wa sekta ya ardhi katika Jiji la Mwanza kwa kuwataka kusimamia sekta hiyo kwa kuzingatia kanuni, taratibu na miongozi ya sekta hiyo.

 

Amesema, kwa kufanya hivyo Wizara ya Ardhi itaweza kuepukana na migogoro ya ardhi isiyo na lazima aliyoieleza kuwa imeendelea kuibuka kila kukicha katika maeneo mbalimbali.

 

Mhe. Pinda alisema hayo tarehe 29 Januari, 2024 alipokutana na wakuu wa idara na vitengo wanaosimamia sekta ya ardhi katika Halmashauri ya Jiji la Mwanza pamoja na wale wa Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Mwanza akiwa katika ziara yake mkoani humo.

 

"Ninyi ndiyo wasimamizi wa sekta hii ya ardhi katika Jiji la Mwanza hivyo mnao wajibu mkubwa wa kufuata kanuni, taratibu na miongozo ya sekta hii ili kuepusha migogoro ya ardhi", alisema mhe. Pinda

 

Amewataka wakuu hao wa idara na vitengo kuwa washauri wazuri wa wakurugenzi wa Halmashauri zao ikiwemo kuzishauri halmashauri kuwa na benki za ardhi katika maeneo yake.

 

"Ninachotaka kuwaambia silka yangu ni kuwapitisha katika maeneo mnayoyasimamia na hii itawasaidia kutekeleza majukumu yenu kwa ufasaha", alisema Mhe. Pinda.

 

Aidha, Naibu Waziri wa Ardhi amehimiza suala la upendo miongoni mwa watumishi wakati wote wa utendaji kazi kwa kuwa ndiyo njia pekee ya kuwawezesha wakuu hao wa idara na vitengo kufanya kazi bila kulaumiwa.

 

Vile vile, Mhe. Pinda amewataka wakuu wa idara na vitengo katika sekta ya ardhi kuwa na mipango madhubuti itakayofanikisha kuzuia ujenzi holela pamoja na kuhakikisha maeneo ya wazi yanalindwa.

 

Amewaasa watendaji hao kuhakikisha wanatatua migogoro ya ardhi katika maeneo yao kwa busara ikiwemo kufanya vikao vya kumaliza tofauti kwa amani.

 

Kwa upande wake Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Mwanza, Happiness Mtutwa alimshukuru Naibu Waziri wa Ardhi kwa kuwafunda na kuwapa elimu na maelekezo na kusema hilo ni jambo muhimu sana katika kuiboresha sekta ya ardhi.

 

Alisema wao kama wakuu wamepokea maelekezo na namna ya kuyashusha kwa watumishi wa chini ili mwisho wa siku maeneo wanayoyasimamia yawe salama.

 

"Nikutoe hofu Mhe. Waziri, ofisi ni taasisi na mara nyingi tumekuwa tukifanyia maelekezo tunayopatiwa na nikuahidi kutekeleza maelekezo na ushauri ulioutoa kwetu kwa kuwa ndiyo msingi wa kuiboresha sekta ya ardhi nchini.’’ Alisema Happy.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi