Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Norway Kuongeza Bajeti ya Kutekeleza Miradi Mbalimbali Nchini
Sep 07, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Waziri wa Norway anayeshughulikia masuala ya Ushirikiano wa Maendeleo ya Kimataifa na nchi za Nordic, Mhe. Anne Beathe Tvinnereim amesema Serikali ya Norway imeongeza bajeti ya kufadhili miradi mbalimbali ya kijamii na maendeleo nchini. 

Waziri Tvinnereim aliyeambatana na ujumbe wake amesema hayo alipozungumza na wakazi wa kijiji cha Chihembe kilichopo Mvumi-Chamwino jijini Dodoma. 

Akizungumza (Jumatano, Septemba 7, 20220) na Wananchi ambao ni wanufaika wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), Waziri Tvinnereim ametaja baadhi ya maeneo ambayo bajeti hiyo itaelekezwa kuwa ni kukabiliana na madiliko ya Tabia Nchi, kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na mpango wa kunusuru kaya maskini nchini kupitia TASAF.

“Natambua na kupongeza kazi kubwa inayofanywa na Serikali ya Tanzania katika kuboresha maisha ya wananchi wake, hata hivyo Serikali ya Norway inatambua changamoto zinazoikabili dunia kwa sasa, kama vile vita vinaovyoendelea kati ya Urusi na Ukraine na COVID-19 ambazo zimepelekea ongezeko la bei ya bidhaa muhimu ikiwemo chakula, mafuta na gesi kwa nchi nyingi duniani ikiwemo Tanzania, hivyo tumeona ni vyema tukaongeza bajeti ya kusaidia miradi na programu mbalimbali za kiuchumi na kijamii zinazotekelezwa Tanzania ili kuwawezesha wananchi kuhimili gharama za maisha”.

Kuhusu kusaidia kubabiliana na mabadiliko ya Tabia Nchi, Waziri Tvinnereim, amesema Norway imesukumwa kusaidia eneo hilo kwa kutambua kuwa asilimia kubwa ya pato la Tanzania linachangiwa na sekta ya kilimo na wananchi wake wengi wamejiajiri katika sekta hiyo huku wakitegemea mvua kuendesha shughuli hizo. 

Ameongeza kuwa ni vyema kuhakikisha uzalishaji katika sekta ya kilimo hauathiriwi na hali ya hewa kwa kukabiliana na Mabadiliko ya Tabia Nchi. 

Akiwa ziarani jijini Dodoma, Waziri Tvinnereim amefanya shughuli mbalimbali ikiwemo kutembelea miradi inayotelezwa na TASAF katika eneo la Mvumi, wilayani Chamwino, sambamba na kutembelea wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya maskini na kuzungumza na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mhe. Dkt. Selemani Jafo na Uongozi wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI). 

Waziri Tvinnereim na ujumbe wake ambaye pia ameambatana na Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Grace Martini yuko nchini kwa ziara ya kikazi ya siku tatu.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi