Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Naibu Waziri Ummy Azindua Kisima cha Maji Safi Pemba
Jan 05, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Na Mwandishi Wetu - OWM

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Watu wenye Ulemavu, Mhe. Ummy Nderiananga amezindua kisima cha maji safi na salama katika shule ya msingi yenye kuhudumia watoto wenye mahitaji maalum ya Mchanga Mdogo iliyopo Wilaya ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Naibu Waziri huyo amezindua kisima hicho ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi Visiwani humo iliyolenga kutembelea na kujionea shughuli za utekelezaji za masuala ya watu wenye ulemavu Pemba tarehe 04, Januari, 2022.

Akiwa amaeambatana na Mbunge wa Jimbo la Kojani na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mhe. Hamad Chande alieleza furaha yake ya uchimbaji wa kisima hicho kitakachosaidia kutatua changamoto za upatikanaji wa maji safi na salama shuleni hapo huku akishukuru wafadhili walioleta huduma hiyo.

“Kipekee niwapongeze Taasisi ya Rehema Foundation na Ofisi ya Mbunge wa Kojani kwa kuchimba kisima na kuonesha umuhimu wa kuleta huduma hii muhimu hasa kwa kundi letu la wenye ulemavu hatua itakayosaidia kuboresha mazingira yao na kuchangia ufaulu wao, kwa hili napongeza sana”, alisema Mhe. Ummy.

Naye Mbunge huyo wa Kojani ambaye pia ni Naibu waziri Ofisi ya Rais Muungano na Mazingira, aliyaeleza furaha yake ya kukamilika kwa maono hayo huku akisema itasaidia kuchagiza utulivu na kusoma kwa bidii.

“Nimpongeze Naibu Waziri kwa kuona umuhimu wa kujumuika na jamii yetu na kuzindua kisima hiki, na kisima hiki ni miongoni mwa visima vitano tulivyoomba Rehema Foundation kuchimba na wameshachimba vinne na leo wamehitimisha cha tano, tunawapongeza,”alisema Mbunge.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Taasisi ya Rehema Foundation, Bw. Mohamed Assa alieleza kuwa, wataendelea kusaidia huduma za kijamii kwa wakazi wa Pemba ikiwa ni sehemu ya kutambua na kuunga mkono jitihada za Serikali na kuwaasa kukitunza ili malengo ya uwepo wa kisima hicho yatimizwe.

Nae Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Bw. Suleiman Kombo alishukuru jitihada za taasisi na ofisi ya Mbunge huku akiwaasa wanafunzi na wakazi wa maeneo hayo kuhakikisha miradi kama hiyo inalindwa na kutunzwa kwani inasaidia kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji kwa jamii kwa ujumla.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi