Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Kandege Aagiza Kituo cha Afya Lubanda Kukamilika kwa Wakati
Jul 19, 2018
Na Msemaji Mkuu

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI) Josephat Kandege jana amefanya ziara ya kikazi Wilaya ya Ileje kukagua ujenzi wa kituo cha Afya cha Lubanda na kuagiza ujenzi wa kituo hicho ukamilike kwa wakati uliopangwa.

Kandege amesema uwepo wa mvua nyingi ambazo huanza mapema katika wilaya hiyo utakwamisha kituo hicho kukamilika mapema endapo hawatautumia muda huu ambao hauna mvua kumalizia ujenzi kwa haraka.

“Ninaamini kama isingekuwa mvua nyingi kunyesha pamoja na kuharibika kwa barabara nimatumaini yangu ujenzi wa kituo hiki cha Afya ungekuwa umekamilika, sasa jitahidini kumaliza haraka kabla ya mvua kuanza, ili mradi huu ukamilike na uanze kuwanufaisha wananchi wa Lubanda na maeneo ya jirani”, amesisitiza Kandege.

Aidha amemuelekeza Mganga Mkuu wa Wilaya ya Ileje Enock Mwambalaswa kubana matumizi ya fedha zilizotolewa kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho ili fedha zitakazobaki zitumike kumalizia jengo  la wazazi na wagonjwa wa nje ambalo lilianza kujengwa kwa nguvu za wananchi pamoja na kujenga nyumba nyingine za watumishi.

Kandege amemuelekeza pia Mhandisi wa Halmashauri ya Ileje kuangalia uwezekano wa kuunganisha wodi ya wazazi na chumba cha upasuaji ili kuendana na ramani mpya za vituo vya afya, aidha ameelekeza utaratibu wa kufikisha umeme kituoni hapo hasa kupita mpango wa REA uanze kufanyika haraka.

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Ileje Haji Mnasi amemueleza Naibu Waziri OR TAMISEMI Josephat Kandege kuwa halmashauri ilipokea shilingi milioni mia tano kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha Afya cha Lubanda na mpaka sasa ujenzi umefikia asilimia 95 na matarajio ni kuwa kituo hicho kitakamilika ifikapo Julai 25, 2018.

Mnasi amemshukuru Naibu Waziri Kandege kwa kufanya ziara ya kukagua kituo hicho na amemuhakikishia kuwa atazingatia maelekezo ya kuwapangia watumishi wapya wa sekta ya afya watakaoajiriwa hivi sasa katika vituo vya afya vinavyojengwa ili vitoe huduma kwa wananchi mara baada ya kukamilika.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi