
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda amewataka watumishi na viongozi wa idara zote ndani ya wizara hiyo kuongeza kasi ya utendaji kazi, akisisitiza kuwa kasi na matokeo ndiyo msingi wa mafanikio ya wizara hiyo.
Akizungumza leo Januari 13, 2026, wakati wa hafla ya makabidhiano ya ofisi kutoka kwa aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi, Makonda amesema mafanikio ya wizara hiyo yatategemea utendaji kazi wa haraka, ubunifu na ushirikiano wa kila mmoja.


“Tofauti yangu na Prof. Kabudi ni kasi. Mimi kazi yangu ni matokeo sasa. Hakuna muda wa kusubiri, kila mmoja akae kwenye nafasi yake, aenee, afunge mkanda, kazi ianze,” amesema Makonda.
Amesisitiza kuwa kila mtumishi lazima aendane na kasi yake ili kuifanya wizara hiyo kuwa kubwa, ya kisasa, na yenye mvuto hata kwa watumishi wa wizara nyingine.


Aidha, Mhe. Makonda amesema anatamani kuona wizara hiyo inajenga kitengo maalum cha mawasiliano ya kimataifa kitakachohakikisha habari na taarifa za nchi zinasambazwa kwa lugha mbalimbali duniani, kwa lengo la kuimarisha taswira ya Tanzania kimataifa.


