Katika mwaka ujao wa fedha 2025/26, Mfuko wa Utamaduni na Sanaa umejipanga kuzidisha ubora na ufanisi wa utoaji wa huduma kwa walengwa pamoja na kushirikiana na wadau katika kutatua kero na changamoto za walengwa ili kuhakikisha wasanii wananufaika na Mfuko huo kama ilivyokusudiwa.
Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Utamaduni na Sanaa Tanzania, Bi. Nyakaho Mahemba ameyasema hayo leo Februari 28, 2025 jijini Dodoma katika ukumbi wa Idara ya Habari – MAELEZO wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa Mfuko huo ndani ya miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita kwa Waandishi wa Habari ikiwa ni programu iliyoandaliwa na Idara hiyo.
Bi. Nyakaho amefafanua kuwa, ushirikiano na wadau unafanyika ikiwa ni utekelezaji maelekezo aliyoyatoa mara kwa mara Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kufanya kazi na wadau hasa walio katika sekta binafsi.
“Mfuko pia umejipanga kuwezesha wasanii wadogo, wachanga na chipukizi kupitia utoaji wa ruzuku ili kuwawezesha kukuza na kuendeleza vipaji vyao na kuwapa nafasi ya kufanya kazi nzuri katika Sanaa na Utamaduni hasa wakati ambapo hawana uwezo wa kifedha wa kufadhili miradi yao”, amesema Bi. Nyakaho.
Mfuko wa Utamaduni na Sanaa umeanzishwa kwa Sheria ya Ujumuisho wa Wadhamini na kuanza kutekeleza majukumu yake mnamo mwezi Desemba 2022 lengo kuu likiwa ni kuinua ubora wa kazi za Utamaduni na Sanaa ili ziweze kujiendesha kibiashara, kuzalisha ajira pamoja na kuchangia katika pato la Taifa.