Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan Aongoza Maelfu Kuaga Miili ya Wanafunzi Jijini Arusha
May 08, 2017
Na Msemaji Mkuu

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amewaongoza maelfu ya Watanzania kuaga miili ya wanafunzi 32, walimu wawili na dereva wa Shule ya Msingi Lucky Vicent waliofariki kwa ajali ya gari Mei 6 mwaka huu Mkoani Arusha.

Katika tukio hilo lililofanyika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Makamu wa Rais ametoa salamu za pole kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli kwa Mkuu wa Mkoa, Wazazi na wote walioguswa na msiba huu.

“Shukrani kwa Rais wa Kenya na Wakenya wote kwa ujumla kwa kujumuika na Watanzania katika kuomboleza msiba huu ulioukumba taifa, ambapo Rais Uhuru Kenyata amemtuma Waziri wa Elimu wa nchi hiyo kuwakilisha Wakenya katika kuomboleza msiba huu” anasema Makamu wa Rais.

Aidha Makamu wa Rais ametoa wito kwa Wizara ya Elimu, Jeshi la Polisi na wazazi kulinda Sheria za Usalama barabarani ili kulinda maisha na ndoto za watoto.

“Msiba huu umegusa kila Mtanzania, hivyo tuzidi kuwaombea Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi, hivyo tujipe moyo na nguvu kwamba hili limetokea na kwa Mwenyezi Mungu tujirudishe” ameongeza Makamu wa Rais.

Hata hivyo Makamu wa Rais ametoa wito kwa madereva wa magari mbalimbali kuwa makini na waangalifu katika vyombo vya moto wanavyovitumia.

Aidha Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Prof. Joyce Ndalichako ametoa pole kwa wazazi wote waliondokewa na watoto na ndugu zao, wafiwa na watanzania wote walioguswa na msiba huo.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Abdulrahman Kinana amewapa pole wazazi na wanajumuia wote na kusema kuwa kama kuna kitu kinatuunganisha sote ni kifo kwani kila binadamu ana mwisho wake.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Freeman Mbowe amesema kuwa Mwenyezi Mungu ametoa nafasi ya kutafakari umoja wetu na ushirikiano wetu kama taifa kupitia msiba huo.

Vilevile Waziri wa Elimu kutoka nchini Kenya Dkt. Fred Matiang’I amesema kuwa Kenya itaendelea kuwa pamoja na Watanzania kwenye kipindi hiki kizito cha msiba huo mzito ulioukumba taifa.

Mbali na hayo Rais Dkt. John Magufuli kwenye ukurasa wake wa Twitter amesema kuwa amepatwa na uchungu na majonzi makubwa alipoyaona majeneza ya watoto na walezi wao waliopoteza maisha katika ajali ya basi huko Arusha.

“Tumepoteza mashujaa wetu katika elimu, tuwaombee na tuendelee kuwa na subira, uvumilivu na ustahimilivu” amesema Rais Magufuli.

Wanafunzi 32, walimu wawili na dereva mmoja wa shule ya Lucky Vicent walipata ajali ya basi Mei 6, mwaka huu Mkoani Arusha walipokuwa wakienda kufanya mtihani wa ujirani mwema.

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi