Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Madaraja ya Korosho Yatambuliwe Kuanzia Ngazi AMCOS - Majaliwa
Nov 22, 2018
Na Msemaji Mkuu

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwaamewaagiza Warajisi Wasaidizi wa Ushirika katika Mikoa yote inayolima korosho nchini waandae semina kwa Maafisa Ushirika, viongozi wa vyama vya msingi (AMCOS), maafisa ugani na wakulima ili kuwawezesha kubaini na kupanga korosho katika madaraja kuanzia ngazi ya vyama vya msingi.

Amesema jambo hilo litasaidia mkulima aweze kujua korosho aliyoipeleka ina ubora gani akiwa huko kijijini na wanapoifikisha kwenye ghala kuu wafanye kazi ya kuthibitisha , kwa hatua hiyo itasaidia kuondoa malalamiko kuhusu madaraja .

“Zoezi hili licha ya kuthibitisha ubora itasaidia kuboresha uzalishaji kwani wakulima wataelimishwa namna ya kuimarisha na kuboresha uzalishaji wa korosho nchini ikiwa ni pamoja na matumizi bora ya viatilifu ’’

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatano, Novemba 21, 2018) wakati alipotembelea kiwanda cha korosho cha BUkO kilichopo kwenye Manispaa ya Lindi, ambapo ameshuhudia korosho zikipimwa ubora kwenye ghala kuu lilipo kiwandani hapo.

Ameagiza semina ifanyike mwakani ili maafisa ushirika baada ya kupata mafunzo wawasaidie wakulima kwenye msimu ujao watambue korosho walizopeleka kuziuza zina ubora gani.

Waziri Mkuu amesema katika semina hiyo wakutane maafisa kilimo na maafisa ushirika ili wapate taaluma hiyo itakayowawezesha kupima korosho na kuitenga katika madaraja na kuwaondolea shida wakati wa mauzo.

Kwa upande wake, Mrajisi Msaidizi wa Ushirika mkoa wa Lindi, Robert Nsunza amemuhakikishia Waziri Mkuu kwamba wataandaa semina hiyo kwa wahusika na kuanzia hapo wakulima wakuwa wakitambua ubora wa korosho zao kuanzia ngazi ya  kijijini.

NayeMkurugenzi wa Kampuni ya Nangomba Holdings, Ramadhan Katau ambaye ndiye mtunzaji wa ghala la korosho katika kiwanda cha BUKO amesema ghala hilo linauwezo wa kupokea na kutunza tani 10,000 za korosho, hadi sasa tani zilizopo ghalani hapo ni 6,370. Hali ya ukusanyaji wa korosho inaendelea kwa kuwa sasa ndio katikati ya msimu .

IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU,

JUMATANO, NOVEMBA 21, 2018.

   

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi