Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Ndg. Gerson Msigwa amewataka Maafisa Habari, Itifaki, Mawasiliano na Uhusiano Serikalini kufikisha taarifa sahihi na kwa wakati kwa wananchi ili wawe na uelewa juu ya mambo mbalimbali yanayotekelezwa na serikali.

Msigwa amesema hayo leo Mei 07, 2026 wakati alipomuwakilisha Waziri wa wizara hiyo, Mhe. Paul Makonda, kufungua Kikao Kazi cha 21 cha Maafisa hao kinachoendelea mkoani Njombe, ambapo amewataka watumie kurasa za mitandao ya kijamii ya taasisi zao na vyombo vya habari kuelimisha Watanzania kazi kubwa inayofanywa na Serikali ili kuepusha madhara ya upotoshaji yanayofanywa na wenye nia ovu.
"Maafisa Habari tumekuwa na kigugumizi kuelezea mambo mbalimbali yanayofanywa na Serikali, matokeo yake tunatengeneza jamii isiyokuwa na taarifa juu ya mambo mbalimbali yanayofanywa na Serikali", alisema Msigwa.

Aidha, amewataka maafisa hao kuendelea kuwaelimisha na kuwahamasisha wananchi juu ya fursa mbalimbali hususani za kiuchumi zinazopatikana katika maeneo yao.