Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Korea Yaipatia Tanzania Trilioni 2
Sep 09, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Na. Josephine Majura na Scola Malinga WFM- Dar es Salaam

Serikali ya Tanzania na Jamhuri ya Korea zimetiliana saini mikopo nafuu ya jumla ya Dola za Marekani bilioni moja sawa na Shilingi trilioni 2.3 kutoka Mfuko wa Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo wa Korea (EDCF) kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo nchini.

Mikataba hiyo imesainiwa jijini Dar es Salaam, kati ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Emmanuel Tutuba kwa niaba ya Serikali ya Tanzania na Balozi wa Jamhuri ya Korea, Mhe. Kim Sun Pyo.

Akizungumza katika halfa ya kusaini mikataba hiyo, Bw. Tutuba alisema kuwa fedha zilizosainiwa zitaenda kutelekeza Mradi wa Upanuzi wa Mfumo wa Vitambulisho vya Taifa awamu ya pili kwa Dola za Marekani milioni 70, sawa na sh. bilioni 163.1

Bw. Tutuba alitaja mradi mwingine utakaonufaika na ferdha hizo kuwa ni Mradi wa Uboreshaji wa miundombinu ya Taifa ya taarifa za ardhi kwa Dola za Marekani milioni 65 sawa na Shilingi bilioni 151.5.

 Mradi wa uendelezaji wa Mifumo ya Usambazaji wa Majisafi na ya Kutibu majitaka kwa Dola za Marekani milioni 70 sawa na Shilingi bilioni 163.1 na Mradi wa Ujenzi wa Chuo cha Kisasa cha mafunzo ya Usafirishaji wa Reli kwa Dola za Marekani milioni 80 sawa na Shilingi bilioni 186.4.

Äidha, Bw. Tutuba alisema fedha zilizosainiwa pia zitatumika katika Ujenzi wa Hospitali ya Binguni, Zanzibar utakaogharimu kiasi cha Dola za Marekani milioni 100 sawa na Shilingi bilioni 233 na kiasi kingine kitatumika kutekeleza miradi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Afya, Nishati na Miundombinu.

“Ninawahakikishia Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, itachukua hatua zote muhimu kuhakikisha ufanisi wa utekelezaji wa miradi yote iliyofadhiliwa kwa fedha za makubaliano haya zinatumika vizuri kufikia malengo yaliyokusudiwa”, alisema Bw. Tutuba.

Naye  Balozi wa Jamhuri ya Korea nchini Tanzania, Mhe. Kim Sun Pyo, amesema kuwa amefurahia kusainiwa kwa mikataba hiyo na kuahidi kuwa Serikali yake itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wake.

 Kwa upande wake Katibu Mkuu  Afisi ya Rais Fedha na Mipango Zanzibar, Dkt. Juma Malik Akil, ameishukuru Jamhuri ya Korea kwa kuendelea kuimarisha ushirikiano na Tanzania kwa kuendelea kufadhili miradi mbalimbali nchini ukiwemo Mradi wa Ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Binguni Zanzibar ambayo inatarajiwa kuwa hospitali kubwa.

Dkt. Akil alisema kuwa Ujenzi wa Hospitali ya Binguni utafungua fursa muhimu katika kuendeleza Sekta ya Afya nchini kwa kuwa ni sekta muhimu katika nguvu kazi na maendeleo ya nchi.

Tangu mwaka 2004 Jamhuri ya Korea kupitia Mfuko wa Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo wa Korea EDCF imeipatia Tanzania kiasi cha Dola za Marekani Milioni 640 zilizotumika katika awamu tatu kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika sekta za miundombinu ya usafirishaji, Elimu, Afya, Nishati na Maji, ikiwemo Ujenzi Mradi wa Ujenzi wa Daraja jipya la Selander linalojulikana kama Tanzanite na Mradi wa Ujenzi wa Miundombinu ya Umwagiliaji Zanzibar.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi