Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Kauli mbiu ya "Nchi Yangu Kwanza" imebeba dhana kubwa kwa Taifa letu-Mhe. Samia Suluhu Hassan.
Dec 09, 2017
Na Msemaji Mkuu

Na Lorietha Laurence - WHUSM, Dodoma.

Makamu Wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.  Samia Suluhu Hassan amesema kuwa Kauli mbiu ya _"Nchi yangu Kwanza"_ya  kampeni ya Uzalendo na Utaifa imebeba dhana kubwa kwa taifa letu.

Mhe. Samia ameyasema hayo leo Mkoani Dodoma alipokuwa akizindua kampeni ya Uzalendo na Utaifa iliyoandaliwa na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo yenye lengo la kukumbusha na kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa kuwa wazalendo.

"Kampeni hii ni muhimu sana katika kuwakumbusha watanzania maana ya uzalendo na umuhimu wa kuudumisha kwa maslahi ya nchi yetu na kizazi kijacho" alisema Mhe. Samia.

Aidha aliongeza kwa kueleza kuwa Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ni kielelezo tosha cha uzalendo kwa namna anavyoyapigania maslahi ya nchi kwa kupiga vita rushwa na matumizi mabaya ya rasilimali ya nchi.

Vilevile Mhe. Samia Suluhu Hassan amemtaka Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt.  Mwakyembe kuunda kamati ndogo za kitaifa zitazozunguka nchi nzima kuhamasisha uzalendo.

Naye Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein ametoa maana ya uzalendo kuwa ni kitendo au hulka ya binadamu kuwa mstari wa mbele kuitetea nchi yake ili kuleta maendeleo.

"Lazima tujitathimini kama kweli tuna uzalendo ndani yetu,  je tupo tayari kusimama na kutetea maslahi ya nchi yetu " alisema Dkt. Shein.

Kwa upande wake Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Mwakyembe aliwashukuru viongozi wa Serikali kwa kuitikia wito na kuunga mkono kampeni hiyo muhimu kwa maslahi ya nchi.

Pia, Dkt. mwakyembe aliahidi kushirikiana na Wizara ya Habari, Utalii Utamaduni   na Michezo ya Zanzibar kuhakikisha kampeni  hiyo inafanyika kwa  kuwawenzi waasisi na wazalendo wa taifa la Tanzania ambao ni Mwl. Julius Kambarage Nyerere na Shekhe. Abeid Amani Karume.

Mbali na hayo, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Bilinith Mahenge ameishukuru Serikali ya Awamu ya tano kuona umuhimu wa kufanyia matukio makubwa ya kiserikali katika Mkoa wa Dodoma na kueleza  kuwa kitendo hicho ni uzalendo wa hali ya juu.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi