Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Kagera Kupata Umeme wa Uhakika 2021
Jul 12, 2017
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_6292" align="aligncenter" width="750"] Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani akisisitiza jambo kwenye uzinduzi wa Mradi wa Usambazaji wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III) katika mkoa wa Kagera[/caption] [caption id="attachment_6290" align="aligncenter" width="750"] Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani (katikati) akibonyeza kitufe kuashiria uzinduzi wa Mradi wa Usambazaji wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III) katika mkoa wa Kagera uliofanyika katika kijiji cha Rwabigaga wilayani Kyerwa. Kulia kabisa ni Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Gissima Nyamo-Hanga na kushoto ni Mbunge wa Kyerwa, Innocent Bilakwate.[/caption]

Na Greyson Mwase, Kagera

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani amesema vijiji na vitongoji vyote vya mkoa wa Kagera vinatarajiwa kupata umeme wa uhakika ifikapo mwaka 2021 kama sehemu ya  utekelezaji wa Mradi wa Usambazaji wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III)

Dkt. Kalemani aliyasema hayo mapema  Julai 11, 2017 kwenye hafla ya uzinduzi wa  Mradi wa Usambazaji wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III) utakaosimamiwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA)  iliyofanyika katika kijiji cha Rwabigaga wilayani Kyerwa mkoani Kagera pamoja na kumtambulisha mkandarasi atakayefanya ujenzi  wa sehemu ya kwanza ya mradi katika mkoa huo.

Alisema utekelezaji wa Mradi wa  Kusambaza  Umeme  Vijijini Awamu ya Tatu katika mkoa wa Kagera utahusisha vipengele  vitatu ambavyo ni pamoja na  kusambaza umeme katika maeneo ambayo hayajafikiwa kabisa na miundombinu ya umeme na kuongeza wigo wa usambazaji  umeme katika  vijiji ambavyo vimefikiwa na miundombinu ya umeme lakini baadhi ya maeneo na vitongoji  havikuungwa.

Waziri Kalemani alisema kipengele cha  tatu kinahusisha usambazaji wa umeme   utokanao na vyanzo vya nishati jadidifu kwenye maeneo yaliyo mbali  na  gridi hususan  visiwani.

Aliendelea kusema kuwa utekelezaji wa mradi huu utatekelezwa kwa vipindi  viwili  tofauti ambapo sehemu ya awali  itahusisha upelekaji umeme katika  vijiji 141 kwa gharama ya shilingi bilioni 45.43 na kuongeza kuwa  utekelezaji wa sehemu ya kwanza ulianza tangu mwezi Februari mwaka huu ambapo inatarajiwa kukamilika mapema Aprili, 2019

Alieleza kuwa kazi hii itafanywa na mkandarasi ambaye ni kampuni ya M/S Nakuroi Investment Company Limited na kuongeza kuwa sehemu ya pili  ya mradi  huu wa kusambaza  umeme vijijini kwa vijiji 180  vilivyobakia  utaanza kutekelezwa baada ya sehemu ya kwanza kukamilika mwaka 2019,  hivyo  kufikisha   umeme katika  vijiji vyote vya mkoa wa Kagera ifikapo mwaka 2021.

Dkt. Kalemani aliwaomba wananchi  kutumia  fursa ya umeme wa uhakika kwa kuboresha maisha yao kupitia miradi ya uzalishaji mali  pamoja na huduma mbalimbali za  jamii ili uwekezaji huu  wa Serikali ulete manufaa yaliyokusudiwa kwa wananchi.

“Wananchi sasa ninawaomba mtumie  fursa hii ya umeme wa uhakika kwa kujenga  viwanda vya kusindika mazao pamoja na huduma za afya, elimu, maji, kilimo na  viwanda vingine, mashine za kusaga, useremala, kuhifadhi vinywaji na  vyakula pamoja na kuchomelea vyuma shughuli  ambazo zitawapatia kipato na kuboresha maisha yenu,” alisisitiza Dkt. Kalemani.

Aidha, Dkt. Kalemani aliwataka wananchi  watakaounganishwa na huduma ya umeme kukamilisha utandazaji wa nyaya  katika nyumba zao mapema ili mkandarasi atakapofika katika maeneo yao wawe tayari kulipia na kuunganishiwa na huduma ya  umeme.

Aliongeza kuwa, wananchi ambao nyumba zao  si kubwa sana wanahimizwa kuomba kufungiwa kifaa maalum kijulikanacho kama  Umeme  Tayari (UMETA) ambacho hakihitaji kutandaza nyaya katika nyumba.

Waziri Kalemani aliwaomba wananchi  kutoa maeneo yao  kwa ajili ya kupitisha miundombinu ya umeme bila ya kudai  fidia kama mchango  wao kwenye mradi huu na  kuwezesha  fedha iliyotengwa kuunganisha wateja wengi zaidi.

Katika hatua nyingine, Dkt Kalemani  aliagiza  Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) katika mkoa wa Kagera kusogeza huduma karibu na wananchi wa wilaya ya Kyerwa ili kuepuka gharama ya  kufuata huduma mbali.

Wakati huo huo akielezea kwa kifupi Mradi Kabambe wa Kusambaza Umeme  Vijijini Awamu ya Tatu, Mkurugenzi Mkuu wa  Wakala wa Nishati  Vijijini (REA) Mhandisi  Gissima Nyamo- Hanga, alisema mradi  unalenga kufikisha huduma ya umeme  kwenye  vijiji 7,873 katika wilaya  na mikoa yote  Tanzania Bara ambavyo bado havijafikiwa na huduma ya umeme.

Alisema kwa mujibu wa taarifa ya maeneo  rasmi ya kiserikali kutoka Ofisi  ya  Rais –Tawala za Mikoa na  Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Tanzania Bara ina  vijiji 12,268 ambapo vijiji  vilivyofikiwa na umeme hadi Juni, 2016 vilikuwa ni 4,395 sawa na asilimia 36.

Mhandisi  Nyamo-Hanga aliongeza kuwa kati ya vijiji 7,873 ambavyo havijapata umeme, vijiji 7,697 vimepangwa kupatiwa umeme wa gridi na vijiji 176 pamoja na visiwa  vitapatiwa umeme wa nje ya gridi kwa kuwa ndiyo njia muafaka ya kuvipatia umeme kwa sasa na kusisitiza kuwa mradi  huu umepangwa kutekelezwa katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka wa fedha 2016/17 hadi 2020/21.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi