Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

JPM Awaapisha Wateule, Awaasa Kuchapa Kazi
Jan 09, 2019
Na Msemaji Mkuu

Na Grace Semfuko.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli  leo Januari 9,2019 amewaapisha viongozi mbalimbali aliowateua Ikulu Jijini Dar Es Salaam na kuwataka kufanya kazi kwa kuzingatia weledi.

Viongozi walioapishwa ni pamoja na Waziri wa Madini Dotto Biteko, Makatibu Wakuu wa Wizara watatu, Manaibu Makatibu wakuu wa Wizara wawili,Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera, Balozi pamoja na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Umma na Makamishna sita wa Tume hiyo.

Akizungumza mara baada ya kuwaapisha viongozi hao Ikulu Jijini Dar es Salaam Rais Magufuli alimtaka Waziri mpya wa Madini Dotto Biteko kusimamia rasilimali za Madini kwa kuanzisha vituo vya madini kwenye mikoa inayofanya shughuli za uchimbaji.

Rais alisema kumekuwa na changamoto kubwa kwenye sekta ya madini ambapotaarifa zinaonyesha   Tanzania kuongoza katika uchimbaji wa Madini katika Nchi za Afrika Mashariki lakini  imekuwa na kiwango cha chini cha uuzaji wa madini kwenye nchi hizo na kuhoji ni kwa nini kumekuwa na hali hiyo.

Ameitaka Wizara ya Fedha na Mipango kwa kushirikiana na Benki kuu ya Tanzania BoT kutenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa dhahabu kwa wachimbaji hatimaye iweze kuuzwa nje kwa fedha za kigeni ili kuiongezea nchi pato la fedha hizo.

“Ripoti mbalimbali katika nchi za Afrika Mashariki zinaonyesha Tanzania kuwa nyuma katika uuzaji wa dhahabu wakati sisi ndio tunaongoza katika uchimbaji, kwa ripoti hii ni lazima tujiulize tunakwama wapi? Dhahabu tunazochimba zinauzwa wapi? Soko lipo wapi na tunalijua? Tunapouza tunapata fedha kiasi gani? Wizara ipo na wataalamu wake na hapo ndio changamoto inapoonekana” Alisema Rais Magufuli.

“Ndio maana wanasema nabadilisha badilisha viongozi, sitaacha kubadilisha na hata Biteko ukifanya vibaya nitakutoa tu na nitaweka mtu mwingine, nafanya hivi kwa ajili ya maendeleo ya Watanzania, sisi tumepewa dhamana lazima tuwatumikie Watanzania” alisema Rais Magufuli

Alisema kwa muda mrefu dhahabu imekuwa hainufaishi nchi ingawa sheria zimerekebishwa lakini bado kumekuwa na changamoto kubwa na kuitaka Wizara ya Madini kusimamia bidhaa hiyo na pia kushirikiana na wachimbaji wengine katika kudhibiti madini hayo muhimu kwa Taifa.

Rais pia alitoa pungezi kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini IGP Simon Sirro kwa kusimamia utoroshwaji wa madini uliofanywa na baadhi ya watu wasio waaminifu wakishirikiana na baadhi ya viongozi wa juu wa Jeshi hilo wanane wa Mkoa wa Mwanza.

“Nikupongeze IGP kwa kusimamia vyema zoezi lile, na wale askari wafanyiwe uchunguzi na kuchukuliwa hatua ikibainika, naomba vyombo vya habari muandike habari zenu kwa uhakika na sio kupotosha, mfano kuna gazeti moja limeandika habari ya kupotosha kuhusiana na kukamatwa kwa dhahabu ile mkoani Mwanza” alisema Rais Magufuli.

Rais pia aliwataka viongozi aliowateua kushirikiana na kuacha migogoro mahali pa kazi na kwamba anatambua baadhi ya maeneo ambayo viongozi hawaelewani na wakati mwiongine kutoleana maneno yasiyofaa huku akitolea mfano kwenye maeneo ya Nyasa, Gairo na Manispaa ya Dodoma.

Kwa upande wake Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa aliwataka viongozi walioapishwa kushirikiana katika kuimarisha maendeleo ya wananchi na kwamba ofisi yake itahakikisha wanapata ushirikiano wa kutosha.

Nae Spika wa Bunge Job Ndugai alimwomba Rais Magufuli kuwapa likizi mawaziri angalau kwa muda ili waweze kupumzika ombi ambalo Rais Magufuli alisema iwapo Watanzania hawana likizo katika ujenzi wa Taifa na mawaziri wanatakiwa kufanya kazi  bila kupumzika.

Jaji Mkuu wa Tanzania Profesa Ibrahim Juma nae alisema Mahakama itashirikiana na viongozi hao katika kuimarisha uhusiano na kufanya kazi kwa kuzingatia weledi.

Viongozi 14 waliapishwa katika hafla hiyo akiwepo Dotto Biteko kuwa Waziri wa Madini ambaye awali alikuwa Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Dkt. Zainab Chaula ameapishwa kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya,maendeleo ya jamii,jinsia wazee na watoto, Dorothy Mwaluko ameapishwa na kuwa Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera na uwekezaji na Elius Mwakalinga kuwa Katibu Mkuu Ujenzi.

Wengine ni Profesa Faustine Kamuzora aliyeteuliwa kuwa Katibu Tawala Mkoa wa Kagera ambaye awali alikuwa Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Dorothy Gwajima kuwa Naibu Katibu Mkuu TAMISEMI na Dkt Francis Michael kuwa Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais menejimenti ya utumishi wa umma na utawala bora.

Aidha Rais pia aliwaapisha Viongozi wa Tume ya Utumishi wa Umma akiwepo Mwenyekiti wa Tume hiyo Jaji Mstaafu Steven Bwana pamoja na Makamishna sita wa tume hiyo akiwepo George Yambesi, Yahya Mbila, Daniel Ole Njoolay, John Haule, Hadija Ally Mohamed Mbarak pamoja na Immaculete Ngwale.

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi