Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

JPM Atoa Milioni 260 Kujenga Makazi ya Polisi Waliounguliwa Nyumba
Sep 29, 2017
Na Msemaji Mkuu

Na: Prisca  Libaga - Maelezo/  Arusha.

RAIS wa Jamuhuri ya muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, ametoa kiasi cha Shilingi milioni 260 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba mpya za askari wa Jeshi la Polisi  Wilaya ya Arusha,zilizoungua Septemba 27 majira ya saa moja usiku na kusababisha familia 14 zenye watu 44 kukosa mahali pa kuishi.

Mkuu wa jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro, amesema mbali na fedha za rais pia jeshi la Polisi limetoa Shilingi milioni 40  kwa ajili ya  ujenzi wa nyumba hizo ambazo ujenzi wake unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Oktoba mwaka huu.

Aidha IGP, amesema jeshi la Polisi limetoa Shilingi milioni moja za kujikimu kwa kila familia iliyounguliwa nyumba.

Akizungumza na askari waathirika wa ajali hiyo ya moto IGP, Sirro alisema Mh.rais ameagiza waathirika hao wapewe nyumba za wakala wa majengo TBA zilizoko Tengeru wilayani Arumeru ili wajisitiri wakati mchkato wa ujenzi wa nyumba zao ukiendelea

Amesema kuwa  kwenye maisha kuna changamoto hivyo ajali hiyo ni sehemu ya changamoto  na ni ajali kama zilivyo ajali nyingine.

IGP Sirro aliwaambia kuwa ametumwa kuwapa salamu za Rais Magufuli pamoja na kuwapa pole  na hivyo watambue kuwa jeshi la Polisi lipo pamoja nao wakati wowote.

Amewaambia kuwa rais alitaka kuwaletea mahema lakini ameamua waathirika wote wakakae kwenye nyumba za Wakala wa majengo zilizopo Tengeru wakisubiri nyumba zao zijengwe.

Amesema hilo tukio lisiwarudishe nyuma wala kuwakatisha tamaa bali  waendelee kuchapa kazi na kutekeleza majukumu yao kama kawaida.

Amewaomba Raia wema kutoa  michango  yao ikiwemo vyakula kwa ajili ya kuwasaidia waathirika wa ajali hiyo ya moto kwani ni jambo la kiungwana na kistaarabu kwa binadamu kusaidiana hasa katika wakati wa shida.

Katika hatua nyingine IGP Sirro na Mkuu wa Mkoa wa Arusha,Mrisho Gambo, wametembelea nyumba za wakala wa majengo ya serikali  TBA zilizopo Tengeru ‘wilayani Arumeru ambazo ndizo zitatumika kwa muda kuhifadhi askari polisi na familia zao waliounguliwa nyumba zao.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi