Serikali kupitia Chuo cha Uhasibu Arusha inaendelea kuchukua hatua za kimkakati kuimarisha mageuzi ya kidijitali katika elimu ya juu, ambapo kupitia chuo hicho imeanza rasmi ujenzi wa Kituo cha Kisasa cha Data kitakachokuwa nguzo ya uhuru wa kidijitali nchini.

Akizungumza leo Februari 20, 2026 katika Ukumbi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mtumba jijini Dodoma, Mkuu wa Chuo cha Uhasibu Arusha, Prof. Eliamani Sedoyeka, amesema hatua hiyo ni sehemu ya mageuzi makubwa ya kimkakati yanayolenga kuifanya taasisi hiyo kuwa kitovu cha maarifa na ubunifu wa kidijitali.

“Katika safari ya kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha maarifa na ubunifu wa kidijitali, IAA imezindua mageuzi makubwa yatakayoongeza uhuru wa kidijitali, ubora wa elimu na ushindani wa kitaifa,” amesema Prof. Sedoyeka.
Amesema uwekezaji huo unatekelezwa kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET), unaofadhiliwa na Benki ya Dunia, ukiweka msingi imara wa mustakabali wa elimu ya juu unaotegemea teknolojia na usalama wa taarifa.

Amesema kituo hicho kitapunguza utegemezi wa upangishaji wa nje, kuimarisha usalama wa mtandao, na kuhakikisha mifumo ya kitaaluma na kiutawala inapatikana muda wote bila hitilafu.
Pia amesema kitasaidia kuhifadhi data za tafiti ndani ya mipaka ya nchi, kuongeza uaminifu wa mifumo ya kidijitali na kuimarisha ulinzi wa taarifa muhimu za taasisi na taifa kwa ujumla.

Prof. Sedoyeka amesisitiza kuwa uwekezaji huo wa kimkakati unaiweka IAA katika nafasi ya kinara wa mapinduzi ya kidigiti katika sekta ya elimu ya juu nchini.