Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

HESLB Yawashukuru Wabunge kwa Kuanza Kurejesha Mikopo.
Jun 07, 2017
Na Msemaji Mkuu

Na Mwandishi Wetu - Dodoma

Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imewashukuru Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao ni wanufaika wa mikopo ya elimu ya juu kwa kuanza kurejesha mikopo yao.

Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Bw. Abdul-Razaq Badru ametoa shukrani hizo leo mjini Dodoma katika maonesho yanayoendelea katika viwanja vya Bunge yenye lengo la kutoa elimu ya urejeshaji wa mikopo kwa waheshimiwa wabunge na watumishi wa Bunge.

“Tunaushukuru uongozi wa Bunge ambao siku zote umekua msaada kwetu katika kuwakumbusha viongozi hawa (wabunge) na watumishi wa Bunge. Tunapata ushirikiano mkubwa sana,” amesema Bw. Badru.

Akifafanua zaidi, Mkurugenzi Mtendaji huyo amesema kufuatia ushirikiano huo, hivi karibuni Spika wa Bunge Mhe. Job Ndugai alielekeza ofisi yake kupatiwa orodha ya wabunge ambao ni wanufaika wa mikopo na tayari orodha hiyo imeshawasilishwa na HESLB kwenye Ofisi ya Katibu wa Bunge ili kuandaa taratibu za kuanza kurejesha.

“Tunahitaji fedha zilizokopeshwa zirejeshwe ili tuwakopeshe watanzania wengine ambao ni wahitaji, hivyo ni muhimu sana kuwakumbusha wadaiwa na ndiyo sababu maafisa wetu wapo hapa,” ameongeza Bw. Badru.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa Urejeshaji Mikopo wa HESLB Bw. Phidelis Joseph ambaye amekuwepo katika maonesho hayo kwa siku zote amesema mwitikio wa Wabunge ni mzuri na wamekuwa wakiuliza maswali mengi ya msingi na kupatiwa majibu kutoka kwa maafisa waliopo katika viwanja hivyo.

Baadhi ya maswali yaliyoulizwa ni pamoja na kuhusu muda ambao mnufaika anapaswa kuanza kurejesha baada ya kumaliza masomo, makato ya asilimia 15 na tozo ya kulinda thamani ya fedha (value retention fee).

Kwa mujibu wa Bw. Joseph, hivi sasa sheria ya HESLB inatoa muda wa miezi 24 kwa mnufaika tangu anapomaliza masomo kurejesha bila adhabu. Aidha, sheria hiyo inamtaka mwajiri kumkata mnufaika asilimia 15 ya msharaha ghafi wa mwezi na kuwasilisha makato hayo kwa HESLB ndani ya siku 15 baada ya mwisho wa mwezi.

Kuhusu tozo la kutunza thamani (Value Retention Fee), Bw. Joseph amesema tozo hiyo inalenga kulinda thamani ya fedha aliyokopeshwa mnufaika ili pale itakaporejeshwa iweze kumsomesha mhitaji mwingine.

Tumepata mrejesho mzuri na tumewaomba kutusaidia kufikisha elimu hii kwa wananchi huko majimboni,” amesema Bw. Joseph.

HESLB ilianza kazi mwaka 2005 ili, pamoja na majukumu mengine, kutoa mikopo kwa watanzania wahitaji na kukusanya mikopo iliyoiva kutoka kwa wanufaika walikoposhwa na Serikali kuanzia mwaka 1994/1995.

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi