Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

EAC Yapata Spika
Dec 20, 2017
Na Msemaji Mkuu

Na mwandishi wetu.

BUNGE la nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA), Desemba 19 limemchagua Martin Ngoga kutoka nchini Rwanda kuwa Spika wa bunge hilo kwa kipindi cha miaka mitano ijayo baada ya kupata kura 33 na kumshinda Joachim Nzeyimana aliyepata kura 3 .

Kulingana na mkataba wa kuanzishwa kwa jumuiya hiyo ilibidi uchaguzi huo uingie awamu ya pili ambapo awamu ya kwanza Ngoga, alipata kura 35 na kuwashinda Nziyimana aliyepata kura moja na Adam Kimbisa wa Tanzania ambae wakati wa uchaguzi hakuwepo ukumbini aliyepata  kura sifuri.

Uchaguzi huo ulisusiwa na wabunge wa Tanzania na Burundi ambao walitoka nje wakati wa kupiga kura ambapo Spika amepigiwa kura na wabunge kutoka Rwanda, Kenya Uganda na Sudani kusini.

Kabla ya uchaguzi huo kufanyika kuliibuka mivutano ya kisheria ambapo wabunge wa Tanzania walieleza kuwa kulingana na mkataba  ulioanzisha jumuiya hiyo  unaeleza kuwa nafasi ya Spika ni ya mzunguko kwa nchi tatu za Tanzania, Kenya na Uganda na hivyo haujafanyiwa marekebishwa ya kuziuhusu nchi nyingine wanachama wapya ambazo ni Sudani kusini, Rwanda na Burundi kuweza kugombea nafasi hiyo.

Waliwataka wabunge hao kuvuta subira kama ambavyo bunge limeweza kukaa kipindi cha miezi sita likisubiri uchaguzi wa wabunge kutoka Kenya hivyo liwe na subira kusubiri Burundi imalize matatizo yake ndipo nafasi hiyo ya Spika  ifanyiwe uchaguzi.

Wabunge wengine walidai kutokuwepo kwa wabunge wa Tanzania na Rwanda hakuzuii kura kupigwa kumchagua Spika  kwa kuwa akidi ya wajumbe kwa mjibu wa mkataba wa kuanzishwa kwa jumuiya hiyo inakidhi matakwa .

Aidha wabunge wengine walitaka suala hilo lifikishwe kwa wakuu wa nchi za Jumuiya ili waweze kulitolea uamuzi .

Hata hivyo wabunge wengine walikataa wakieleza kuwa bunge ni mamlaka kamili hivyo ina uwezo wa kufanya maamuzi kama muhimili  na hawachaguliwi Spika na muhimili mwingine.

Desemba 18 mbunge mmoja aliweka pingamizi kuzuia Tanzania isipewe nafasi hiyo ya kugombea nafasi ya Uspika kwa sababu tayari walishawahi kupata nafasi hiyo hivyo zamu ipewe wanachama wapya.

Iwapo nchi zote zingeshiriki kwenye uchaguzi huo wa Spika zingelipigwa kura 54 ,kutokana na Tanzania na Burundi kutoshiriki zimepigwa kura 3

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi