Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

BOT yaanza kufuta Maduka ya Kubadilishia Fedha Yasio na Leseni
Feb 28, 2019
Na Msemaji Mkuu

Tarehe 27 Februari 2019 Benki Kuu ya Tanzania ilifanya ukaguzi wa kawaida wa maduka ya kubadilisha fedha za kigeni jijini Dar es Salaam na kubaini kwamba maduka mengi yanaendesha biashara hiyo pasipo kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za utoaji wa huduma ya kubadilisha fedha za kigeni.

Kufuatia ukaguzi huo, Benki Kuu ya Tanzania imeanza utaratibu wa kufuta leseni za maduka yote yaliyokutwa yanaendesha biashara hiyo bila kuzingatia masharti ya leseni. Zoezi hili linaendelea.

Mnamo mwezi Desemba mwaka 2018, Benki Kuu ya Tanzania ilifanya ukaguzi wa maduka ya kubadilisha fedha za kigeni nchini kote na kubaini kuwa mengi hayakidhi matakwa ya kisheria ya biashara hiyo. Hivyo, iliyaandikia maduka hayo kuyataka kutoa maelezo kwa nini yasifutiwe leseni kutokana na ukiukaji huo. Hatua zilizochukuliwa jana zinatokana na tathmini ya taarifa ambazo Benki Kuu ya Tanzania ilizipokea kutoka kwa waendeshaji wa maduka hayo.

Aidha, kama ilivyoelezwa katika taarifa za Benki Kuu ya Tanzania za mwezi Novemba 2018 na tarehe 31 Januari 2019, huduma za kubadilisha fedha za kigeni zinaendelea kupatikana katika mabenki na taasisi za fedha nchini kote pamoja na maduka ya fedha za kigeni ya Shirika la Posta Tanzania (TPC).

Benki Kuu ya Tanzania inapenda kuutahadharisha umma kutotumia huduma zisizo rasmi za ubadilishaji wa fedha za kigeni kutokana na hatari mbalimbali, ikiwemo kuibiwa au kupewa fedha bandia. Aidha, utumiaji wa huduma zisizo rasmi ni kinyume cha sheria za nchi. Hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya watoaji na watumiaji wa huduma zisizo halali (black-market).

Imetolewa na:

Idara ya Uhusiano wa Umma na Itifaki

botcommunications@bot.go.tz

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi