Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Bilioni 3.7 Zachangwa Kuziwezesha Timu za Taifa
Jan 10, 2024
Bilioni 3.7 Zachangwa Kuziwezesha Timu za Taifa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, akizungumza na wadau wa michezo nchini kupitia simu ya mkononi kwenye Harambee ya kuchangia timu za taifa zinazoshiriki michuano ya kimataifa, iliyofanyika katika ukumbi wa Johari Rotana, jijini Dar es Salaam, Januari 10.2024, ambapo kiasi cha shiLingi bilioni 3.7 zilipatikana.
Na Ofisi ya Waziri Mkuu

Zaidi ya shilingi bilioni 3.7 zimechangwa ikiwa ni fedha taslimu na ahadi katika hafla ya kuzichangia timu za Taifa za Tanzania ambapo kati ya hizo Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amechangia shilingi milioni 500.

 

Fedha hizo zilipatikana kutokana na wadau kutoka sekta mbalimbali ikiwa ni pamoja na wizara na taasisi za Serikali, taasisi za kifedha, mashirika ya hifadhi za jamii, wafanyabiashara na wasanii pamoja na njia ya mnada ambapo jezi zenye majina ya wachezaji wa timu ya Taifa iliyoshiriki AFCON miaka ya 1980 ziliuzwa na jezi iliyouzwa na gharama kuwa ilikuwa ya golikipa Juma Pondamali iliyonunuliwa kwa shilingi milioni 25.

 

Mheshimiwa Rais Dkt. Samia ametoa mchango huo jana usiku Jumatano, Januari 10, 2024 wakati alipompigia simu Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwa ajili ya kuzungumza na wadau mbalimbali wa michezo waliojitokeza katika hoteli ya Johari Rotana jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuzichangia timu za Taifa.

 

“Wito wangu na ombi langu kwenu Watanzania wenzangu tuchangie timu zetu ili ziende kuwakilisha vizuri jina la Tanzania. Serikali imejitahidi na imehamasisha na timu zetu zinasonga mbele, michezo ni gharama ndugu zangu. Mimi na marafiki zangu kwa kuanzia tutachangia shilingi milioni 500.”

 

Waziri Mkuu ambaye aliongoza harambee hiyo kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia alisema lengo la kukusanya fedha hizo ni kuziwezesha timu za Taifa zinazoshiriki katika michuano mbalimbali ya kimataifa kusonga mbele. “Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi thabiti wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tumeshuhudia mageuzi makubwa sana katika sekta ya michezo.”

 

Waziri Mkuu alisema mageuzi hayo yametokana na jitihada na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali pamoja na wadau mbalimbali yakiwemo makampuni pamoja na watu binafsi, ambapo utashi mkubwa wa kisiasa katika sekta ya michezo umeleta msukumo chanya unaoongeza ari na morali kwa wadau wa sekta ya kuunga mkono na kuzienzi jitihada za Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika uwekezaji na mabadiliko makubwa katika sekta ya michezo.

 

Alisema kwa upande wa mpira wa miguu, Timu ya Taifa ya Mpira wa Miguu ya Wanaume “Taifa Stars” imefuzu kucheza mashindano ya AFCON yanayofanyika nchini Ivory Coast mwezi huu Januari 2024. “Ninayo furaha kuwataarifu kuwa hivi sasa timu yetu ipo kambini nchini Misri na tayari Mheshimiwa Rais ameshatoa fedha za kusaidia Timu ya Taifa kushiriki mashindano haya.”

 

Vilevile, Waziri Mkuu alisema Timu ya Taifa ya Wanawake ya Mpira wa Miguu “Twiga Stars” imefuzu kucheza mashindano ya WAFCON ambayo yatafanyika mwaka huu nchini Morocco, timu hiyo nayo imepewa bonasi ya Mheshimiwa Rais ya shilingi milioni 200 ilipofuzu mashindano hayo.

 

Awali, Mwenyekiti wa kamati ya hamasa ya kuchangia timu za Taifa, Bw. Theobaid Sabi alisema kamati yao ina majukumu makuu matatu ambapo la kwanza ni kutafuta fedha kwa ajili ya kugharamia timu za Taifa zinazotarajia kushiriki mashindano ya kimataifa, kuuelimisha umma kuhusu uwepo na umuhimu wa Timu za Taifa na kuuhamasisha kuziunga mkono na kuzichangia timu hizo.

 

Bw. Sabi ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya NBC alisema lengo ni kukusanya shilingi bilioni 10, hivyo amewaomba wadau wajitokeze kwa hali na mali kuchangia timu hizo. Alisema Benki ya NBC itaanza kuchangia shilingi milioni 100.

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi