Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Ardhi Ni Akiba Ambayo Thamani Inaongezeka Kila Siku Msiuze Ovyo – RC Tabora
Aug 09, 2017
Na Msemaji Mkuu

Na: Tiganya Vincent, RS-Tabora

Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw. Aggrey Mwanri amewaonya wakazi mkoani hapa kuacha tabia ya uuzaji ovyo wa ardhi huku wao wakibakiza eneo dogo la ardhi wanalolimiki ambalo haliwezi kutosheleza matumizi ya familia zao katika siku za baadaye.

Kaulu hiyo ilitolewa jana na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw. Mwanri kwenye sherehe za kilele cha maonesho ya nane nane kwa kanda ya Magharibi yalifanyika katika Viwanja vya Fatuma Mwasa mjini hapa.

Alisema kutokana na  Mkoa wa Tabora kuanza kufunga kwa kasi kwa kuwa na miundo mbinu mbalimbali kama vile usafiri wa uhakika wa anga , kuanza ujenzi wa mradi mkubwa wa maji kutoka ziwa Victoria, ujenzi wa reli ya kisasa na barabara za lami zinaongeza fursa ya watu mbalimbali kuja mkoani hapa kwa shughuli mbali.

Bw. Mwanri alisema watu hao wanaweza wakajitokeza na kuanza kuwarubuni wakazi ili wawauzie ardhi zao hata kwa bei ambayo halingani na eneo husika huko wenyewe wakipata fedha kidogo ambazo hazimsaidii kujiendeleza bali kuendelea kuwa maskini.

Mkuu huyo wa Mkoa alisema kuwa thamani ya ardhi inaongezeka kila siku na watu wanaohitaji wanaongezeka na hivyo ni vema wakawa makini kabla ya kufanya maaumuzi  ya kuuza vipande vyao vya ardhi ili wasije wakajuta mara fedha walizolipwa zitakapokuwa zimekwisha.

Aliongeza kuwa hata kama mtu anataka kuuza eneo lake ni vema akajihakikishia kuwa lilobaki litaiwezesha familia yake kuwa na mahali bora pa kuishi na kufanyia shughuli nyingine za uchumi kama vile kilimo na ufugaji wa kisasa.

Bw. Mwanri alisisitiza kuwa uuzaji wa ovyo wa ardhi ndio wakati mwingine umepelekea migogoro pindi wauuzaji wanapokuwa wamemaliza fedha walizolipwa huku wao hawajafanya kitu na kuunza kuvamia maeneo ya wengine.

Mmoja wa Wakazi wa Tabora Bi. Rebecca Alfred anapongeza hatua ya Mkuu wa Mkoa kutoa angalizo hilo kwa wakazi wa Mkoa huo na kusema kuwa migogoro mingi katika familia imesababishwa na baadhi ya ndugu kuuza maeneo yao na wanapomaliza eneo yao wanaanza kuvamia ya maeneo ya wenzao.

Alisema kuwa njia pekee ya kuondoa matatizo hayo ni pamoja na kupima maeneo yote ya wananchi na kuwapa hati ambazo wanaweza kunufaika na huduma za mikopo kwa ajili ya shughuli mbalimbali za maendeleo.

Bi. Rebecca alitoa wito Watendaji wa Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge nchini(MKURABITA) kuhakikisha wanaharakisha kupima mashamba ya wananchi na kutoa elimu juu matumizi bora ya ardhi ili kuwasaidia waweze kutumia ardhi yao kupata mikopo badala ya kuuza kama sehemu ya kutafuta fedha na kila mtu kujua mipaka yake.

Alisisitiza amesikia maeneo ambayo MKURABITA wamepima mashamba ya wananchi kumekuwepo na maendeleo hata kwa wananchi na wamejua thamani ya ardhi na hakuna uuzaji ovyo ovyo.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi