Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Waziri Mkuu Azindua Jukwaa La Biashara Na Uwekezaji Tabora
Nov 22, 2018
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_38652" align="aligncenter" width="750"] Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza wakati alipozindua Jukwaa la Fursa za Biashara na Uwekezaji Mkoani Tabora kwenye ukumbi wa Mkuu wa Mkoa huo, Novemba 21, 2018.[/caption]

Awaagiza viongozi wa mikoa nchini wabaini fursa walizonazo na wazitangaze.

Waziri Mkuu amewaagiza viongozi wote wa mikoa nchini wahakikishe wanashirikiana na makundi yote kuzibaini fursa zilipo katika maeneo yao, kuziorodhesha na kuzitangaza kwenye vyombo vya habari na majukwaa ya biashara na uwekezaji ili zipate wawekezaji haraka.

Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo leo (Jumatano, Novemba 21, 2018) wakati akizindua Jukwaa la Fursa za Biashara na Uwekezaji la Mkoa wa Tabora, ambapo ameagiza fursa zote ziandaliwe na kuandikwa vizuri ili wenye mitaji kutoka ndani na nje waweze kuziona na kuja kuwekeza.

Pia Waziri Mkuu amewataka Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri mkoani Tabora na watendaji wote wa Serikali wawajibike kwa wananchi kwa kusikiliza kero zao na kizitatua kero zote zinazochelewesha biashara na uwekezaji katika maeneo yao.

Kadhalika Waziri Mkuu amezitaka idara zote za Serikali katika ngazi za mikoa na wilaya zishirikiane na kubununi njia rahisi zitakazosaidia kuzijua fursa zilizopo kwenye maeneo yaona kuzitangaza ili kusaidia upatikanaji wa ajira kwa vijana wanaomaliza shule, vyuo na vyuo vikuu kwa kujiajiri wenyewe.

Amesema Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli imedhamiria kujenga uchumi wa viwanda ili Taifa lifikie uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025. “Viwanda vinalenga  kutengeneza ajira nyingi kwa akina mama na vijana na kuiwezesha Serikali kupata fedha za kigeni zitokanazo  mauzo ya bidhaa ndani na nje ya nchi .”

Waziri Mkuu amesema fedha hizo za kigeni ni muhimu sana katika kuiwezesha Serikali kutekeleza mipango na miradi mbalimbali ya maendeleo kama ile inayoendelea sasa ya ujenzi wa reli ya kisasa (SGR), Stiegler’s Gorge, miradi ya usafirishaji umeme na mingineyo.

“Ubunifu na mipango ya namna hii inayotekelezwa na Mkoa wa Tabora inakwenda bega kwa bega na dhamira ya Mheshimiwa Rais wetu mpendwa na watendaji wengine wote wa Serikali katika kuhakikisha tunafikia uchumi wa viwanda.

Kadhalika, sote tumesikia fursa zilizopo Mkoani Tabora zikiwemo maliasili kama vile misitu, mbao, uzalishaji wa asali pamoja na kilimo cha tumbaku, pamba, alizeti na shughuli nyingine nyingi za ujasiriamali mdogo na wa kati.”

Pia, Waziri Mkuu ametaja fursa mpya zinazojitokeza mkoani Tabora ambazo ni bomba la mafuta ghafi linalotoka HOIMA nchini Uganda kwenda Tanga ambalo litapita mkoani humo pamoja na ujenzi wa reli ya kisasa (SGR).

Amesema hizo ni miongoni mwa fursa zitakazousaidia mkoa wa Tabora ujulikane zaidi, hivyo kuibua uhitaji wa uwekezaji zaidi katika shughuli za kibenki, hoteli, huduma za mikutano na starehe, maeneo ya michezo, shule na shughuli nyinginezo. “Mambo yote haya yataibua fursa lukuki za uwekezaji mkoani Tabora.”

Waziri Mkuu amesema Serikali kwa upande mwingine inaendelea na jitihada kubwa za kuunganisha mikoa yote na mtandao wa barabara za lami ukiwemo mkoa wa Tabora kwa kuwa kuimarika kwa miundombinu usafirishaji ndani na mikoa ya jirani, kutatoa fursa nzuri katika kuifungua Tabora na kuleta mwelekeo mpya wa kiuchumi na kijamii.

“Nitoe rai kwa uongozi mzima wa Mkoa wa Tabora kuendeleza kazi hii nzuri mnayoifanya kwa wana Tabora na msirudi nyuma. Endeleeni kuwa wabunifu zaidi, shirikisheni makundi yote ya kijamii ili kupanga na kutekeleza mambo haya kwa pamoja.

Hakikisheni mnatoa kipaumbele kwa akina mama na vijana katika kuwasaidia mitaji na elimu kwa lengo la kuinua na kuimarisha shughuli zao za kiuchumi na kijamii. Kufanya hivyo, mtawezesha jamii inayowazunguka kunufaika haraka na mipango yenu ya maendeleo.”

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameipongeza Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) kwa kazi nzuri inayofanya ambapo tayari wameshakwenda mikoa saba nchini Tanzania Bara na Zanzibar wakisaidia kuziibua fursa, kuziandika kwenye vyombo vyao na pia kuzitangaza kupitia majukwaa hayo wanayoyaandaa, ambayo yamesaidia sana kupata wawekezaji mbalimbali. Mkoa wa Tabora ni mkoa wa nane.

“Niwaombe TSN mshirikiane na mikoa mingine  kuandaa na kuhimiza majukwaa haya ya fursa za biashara na uwekezaji. Ni matumaini yangu  kuwa kila baada ya jukwaa kama hili kutafanyika tathmini za kina ili kupima matokeo yaliyotarajiwa.”

Waziri Mkuu ametoa wito kwa TSN baada ya kukamilisha majukwaa katika ngazi za mikoa waangalie uwezekano wa kuandaa majukwaa kama hayo kwenye ngazi za wilaya na kisekta, ambapo ametolea mfano sekta za kilimo, madini, ufugaji au ujasiriamali ili wasaidie kuziibua na kuzitangaza fursa zilizopo kwenye sekta hizo kama wanavyofanya sasa.

[caption id="attachment_38672" align="aligncenter" width="750"] Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa Saidi Kanimba kuhusu viatu vya ngozi vinavyotengenezwa katika Halmashuri ya wilaya Uyui mkoani Tabora katika Maonyesho ya Jukwaa la Fursa za Biashara na Uwekezaji Mkoani Tabora yailyofanyika kwenye Viwanja vya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Novemba 21, 2018. Kushoto kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri.[/caption] [caption id="attachment_38674" align="aligncenter" width="750"] Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akitazama sabuni za Kampuni ya Matabula Soap Investment ya Kaliua mkoani Tabora, Imani Matabula (kulia) katika maonyesho ya Jukwaa la Fursa za Biashara na Uwekezaji Mkoani Tabora yaliyofanyika kwenye viwanja vya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Novemba 21, 2018. Katikati ni Mkuu wa Mkoa huo, Aggrey Mwanri. Wapili kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri na kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni hiyo, Imani Matabula.[/caption] [caption id="attachment_38676" align="aligncenter" width="750"] Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akitazama chupa yenye ujazo wa nusu lita yA mkojo wa sungura wakati alipotembelea banda la wanawake wajasiriamali wasindikaji wa Tabora katika maonyesho ya Jukwaa la Fursa za Biashara na Uwekezaji katika Mkoa wa Tabora yaliyofanyika kwenye viwanja vya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Novemba 21, 2018.
Kwa mujibu wa Mratibu wa Wajasiriamali hao, Bibi Ashura Mwazembe, mkojo wa Sungura unatumiwa kama mbolea ya mazao ya kilimo na pia ni dawa nzuri sana ya kuua wadudu waharibifu wa mazao. Lita moja ya mkojo huo inauzwa sh. 10, 000/=. (Picha na ofisi ya Waziri Mkuu)[/caption]  

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi