Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Waziri Jafo Atoa Wito Kulinda Rasilimali za Bonde la Mto Nile
Aug 19, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Selemani Jafo amefungua Mkutano ya Mabaraza ya Mawaziri wa Maji wa Nchi za Bonde la Mto Nile jijini Dar es Salaam leo Agosti 19, 2022.

Akifungua mkutano huo kwa niaba ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango, Waziri Jafo alitoa wito wa kulinda rasilimali za Bonde la Mto Nile ili zilete manufaa kwa wananchi wanalolizunguka.

Alisema ushirikiano ni njia bora katika kusimamia kwa amani rasilimali zetu za maji, hivyo mikutano ya Mawaziri wa Bonde la Mto Nile inatoa fursa ya kutafakari na kufanya kazi pamoja na kuweka misingi ya ushirikiano na kutoa maelekezo ya kisera kuhusu usimamizi wa rasilimali hiyo.

Dkt. Jafo alisema ingawa nchi zinapakana lakini maji hayana mipaka na hivyo tuna kila sababu ya kulinda rasilimali hii akitolea mfano, kufikia sasa kuna zaidi ya mabonde maji shirikishi 276 duniani likiwemo Bonde la Mto Nile na sehemu ya mabonde hayo inachukua nusu yaardhi ya dunia.

Alitoa rai kwa nchi wanachama kuhakikisha kuwa suala la kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi na kulinda vyanzo vya maji liwe endelevu katika mikakati ya kila siku.  

“Tuna kila sababu ya kulinda bonde hili na endapo chanzo hiki muhimu na adimu ambacho Mungu ametupatia endapo kitaathirika hatuna mbadala badala yake tunapaswa kukilinda na kukiendeleza na ndio maana tunafanya mikutano hii tuweze kujadiliana,” alisema.

Hata hivyo, alisema kuwa changamoto ya mabadiliko ya tabianchi imekuwa ni kubwa hivyo nchi zote wanachama zinapaswa kushirikiana ili kupambana nayo kwani ikiathirika nchi moja zinaathirika zingine.

Alisema Tanzania chini ya Rais Samia Suluhu Hassan inatekeleza miradi ya mbalimbali ya kimkakati ambayo inasaidia katika kupambana na athari za mabadiliko yatabianchi. Pia aliipongeza Wizara ya Maji kwa kutekeleza miradi inayosaidia katika kupambana na mabadiliko ya tabianchi.

Aidha, wakati akizindua Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Bonde la Mto Nile jiji Dar es Salaam Februari mwaka huu, Makamu wa Rais Mhe. Dkt. Mpango alikumbusha kuwa miaka 20 sasa tupo katika safari ya kuanzisha Kamisheni ya Bonde la Mto Nile.

Waziri Jafo aliweka msisitizo katika suala la utekelezaji wa maelekezo hayo na kuwakumbusha nchi wanachama kuwezesha Sekretarieti ya Bonde la Mto Nile iweze kufanya kazi iliyokusudiwa.

Mkutano huo umehudhuriwa na viongozi wa nchi wanachama wa Bonde la Mto Nile zikiwemo Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Misri, Ethiopia, Kenya, Rwanda, Sudan na Uganda.

Kwa mwaka huu Tanzania imepewa heshima ya kuwa mwenyeji wa mkutano huo na kupokea Uenyekiti wa Baraza hilo kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi