Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Serikali Yaongeza Ushiriki wa Vijana, Wanawake Shughuli za Kilimo
Aug 08, 2023
Serikali Yaongeza Ushiriki wa Vijana, Wanawake Shughuli za Kilimo
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Dkt. Amos Nungu kuhusu Tume hiyo inavyowasaidia wakulima wenye ubunifu mbalimbali katika Maonesho ya Kimataifa ya Wakulima Nane Nane yaliyofanyika kwenye viwanja vya John Mwakangale Jijini Mbeya tarehe 8 Agosti, 2023.
Na Jonas Kamaleki - Mbeya

Serikali inaendelea kufanya juhudi za makusudi ya kuongeza ushiriki wa vijana na wanawake katika sekta ya kilimo ili kuwaletea maendeleo yatokanayo na kilimo.

Kauli hiyo imetolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan leo jijini Mbeya wakati wa Kilele cha Maonesho ya Siku ya Wakulima ( Nanenane) yaliyofanyika kitaifa jijini humo.

Rais Samia amesema zipo programu na juhudi za makusudi za kuwawezesha wanawake na vijana katika kilimo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, akiwa na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Tulia Ackson, Waziri wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Juma Homera, Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Gerald Mweli pamoja na Dkt. Hussein Mohammed Omar ,Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo wakati akikata utepe kuashiria uzinduzi wa ugawaji wa vifaa vya maafisa ugani, trekta kwa wakulima, vifaa vya kutengeneza Vihenge vya chuma kwa Vijana, bei elekezi za mbolea ya ruzuku, mradi wa uchimbaji wa visima pamoja na ugawaji wa vifaa vya mfumo wa umwagiliaji kwa matone katika Maonesho ya Kimataifa ya Wakulima Nane Nane yaliyofanyika Kitaifa Mkoani Mbeya tarehe 8 Agosti, 2023.

 

"Miongoni wa juhudi hizo ni kuanzishwa kwa programu ya miaka 8 inayoitwa "Jenga Kesho Iliyobora"  ambapo hadi sasa vijana 812 wanakidhi vigezo ikiwa ni wanawake 282 na wanaume 530 wanaendelea na mafunzo ya awamu ya kwanza," alisema Rais Samia.

Aliongeza kuwa baada ya kuhitimu mafunzo hayo vijana watapatiwa mashamba yenye kufikia hadi ekari 10 kulingana na mazao wanayokwenda kulima, mashamba hayo watakodishwa kwa miaka 66.

Juhudu zingine za makusudi ni serikali inaendelea kutafuta wawekezaji watakaokuwa wakinunua mazao hayo na kuyaongezea thamani.

Kwa mujibu wa Dkt. Samia juhudi hizi zimeifanya Tanzania kujulikana kimataifa na kuchaguliwa kuwa mwenyeji Jukwaa la Kilimo litakalofanyika Septemba 5 hadi 8, 2023.

Kufuatia jukwaa hilo Tanzania itapata fursa za kibiashara na kuimarisha mashirikiano na nchi za Afrika kwenye mifumo ya chakula.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi