Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Mapato Sekta ya madini yaongezeka Maradufu
Oct 23, 2018
Na Msemaji Mkuu

 

Mapato yanayotokana na madini ya Tanzanite yameongezeka kutoka milioni 166 mwaka 2015 hadi zaidi ya shilingi bilioni 1.28 kwa kipindi cha Januari hadi Septemba 2018.

Akizungumza  katika kipindi cha “TUNATEKELEZA” Waziri wa Madini Mhe. Angellah Kairuki amesema kuwa kuongezeka kwa mapato hayo ni matokeo ya hatua zilizochukuliwa na Serikali ikiwemo ujenzi wa ukuta katika eneo la Mirerani na kuimarishwa kwa ulinzi katika viwanja vya ndege na maeneo yote ya mipakani kuzuia utoroshaji wa madini.

“Serikali imejipanga kuhakikisha kuwa mchango wa sekta ya madiniunaongezeka kutoka asilimia 4.8 kwa sasa hadi kufikia asilimia 10 mwaka 2025;” Alisisitiza Mhe. Kairuki

Akifafanua amesema kuwa Serikali imejipanga kuongeza mapato yanayotokana na madini kwa ujumla kutoka bilioni 301 mwaka 2017/2018 hadi bilioni 310 mwaka 2018/2019.

Aliongeza kuwa katika kuimarisha uwekezaji katika sekta hiyo Wizara ya Madini imendaa makongamano katka nchi za China, Urusi, Israel, India, Thailand, na Falme za Kiarabu ili kuvutia wawekezaji katika sekta ya madini hali itakayosaidia kukuza na kuongeza mchango wake katika pato la Taifa.

Kutokana na marekebisho ya Sheria  ya madini yaliyofanyika na kutungwa kwa sheria mpya  katika usimamizi wa rasilimali za Taifa kumewezesha mrabaha kuongezeka kutoka asilimia 4 hadi 6 kwa sasa.

Akizungumzia wachimbaji wadogo Mhe. Kairuki amesema kuwa Serikali imewatengea zaidi ya maeneo 46 ili kuwapa fursa ya kushiriki katika ujenzi wa uchumi kupitia katika sekta ya madini.

Pia alieleza kuwa Serikali inawajengea uwezo wachimbaji hao ili waweze kuwa na mbinu za kisasa za uchimbaji, uongezaji thamani na uzingatiaji wa sheria zilizopo kwa manufaa yao na Taifa kwa ujumla.

Katika kuimarisha sekta hiyo, Mhe. Kairuki amebainisha kuwa tayari Wizara yake imeanza mchakato wa kuhakikisha kuwa madini ya Tanzanite yanapata hati miliki ikiwa ni utambulisho rasmi kuwa madini hayo yanatoka Tanzania pekee hali itakayoongeza mapato kutokana na madini hayo.

Kipindi cha “TUNATEKELEZA” kinaratibiwa na Idara ya Habari MAELEZO na kurushwa na Shirika la Utangazaji Tanzania na awamu hii inawashirikisha Waheshimiwa Mawaziri wote.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi