Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Makamu wa Rais Akutana na Viongozi wa Waahmadiyya
Aug 15, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango leo tarehe 15 Agosti 2022 amekutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa Jumuiya ya Waislamu Waahmadiyya nchini Tanzania wakiongozwa na kaimu Amiri wa Jumuiya hiyo, Sheikh Abdulrahaman Ame, mazungumzo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es salaam.

Katika mazungumzo hayo, Makamu wa Rais ameipongeza na kuishuuru Jumuiya hiyo kwa kuendelea kuiunga mkono Serikali pamoja na kuiombea nchi na viongozi wake. Amesema Serikali inatambua mchango wa Jumuiya hiyo katika kutatua changamoto mbalimbali za wananchi hususani katika sekta ya afya, elimu, maji na nishati ya umeme.

Makamu wa Rais ameiasa taasisi hiyo pamoja na viongozi wengine wa dini kuweka mkazo katika kusimamia maadili hususani kwa vijana kutokana na athari zitokanazo na mitandao ya kijamii hivi sasa. Pia amewasihi kuendelea kuhimiza waumini kufanya kazi ili kuleta maendeleo kwao na kwa taifa kwa ujumla. Makamu wa Rais amesema dini zinapaswa kuwa chanzo cha upendo na umoja baina ya watanzania na hazipaswi kutumika kama chanzo cha chuki baina ya waumini.

Pia amewasihi viongozi hao kusisitiza waumini kushiriki katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi inayotarajiwa kufanyika Agosti 23 mwaka huu. Amesema Serikali itaweza kupanga na kutekeleza mipango ya maendeleo pamoja na kufahamu namna ya kugawa rasilimali kama idadi ya watu na maisha yao itafahamika kupitia sensa.

Awali akitoa taarifa ya maendeleo ya Jumuiya ya Waislamu Waahmadiyya Tanzania, Katibu wa Jumuiya hiyo, Sheikh Seif Nakuchima ameishukuru Serikali kwa kuendelea kudumisha misingi ya amani pamoja na kutoa uhuru na kusimamia ili kila mwananchi aweze kutekeleza Imani yake pasipo kubughudhiwa.

Amesema  Jumuiya hiyo inaendelea na kazi ya kuhamasisha amani hapa nchini ikiwemo kuanzisha siku ya waanzilishi wa dini ambayo imelenga kuchagiza amani pamoja na kuandaa mikutano inayolenga kuhimiza wananchi kuishi kwa amani, kuheshimiana na kuvumiliana kwa watu wa dini zote na jamii zote. Amesema katika mikutano hiyo hushirikisha viongozi wa serikali, vyama vya siasa na vyombo vya usalama ili kuweza kuweka misingi imara ya amani katika maeneo husika.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi