Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Hospitali ya Rufaa ya Bombo Yapokea Msaada wa Maabara ya Kisasa kutoka Serikali ya Ujerumani
Aug 16, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Na Oscar Assenga, TANGA.

Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga Bombo imepokea msaada wa maabara ya kisasa ya kufanyia uchunguzi wa ugonjwa wa UVIKO - 19 yenye thamani ya Shilingi milioni 225 kutoka kwa Serikali ya Ujerumani kupitia Shirika lake la Maendeleo ya GIZ

Akizungumza mara baada ya kuifungua na kukagua maabara hiyo, Waziri wa Afya Ummy Mwalimu alisema kwamba maabara hiyo ina uwezo wa kutoa majibu ndani ya masaa nane, hivyo kuwa mwarobaini wa changamoto zilizokuwepo awali.

Alisema kuwa pia kupitia uwepo wa maabara hiyo utasaidia hata wananchi kutoka nchi jirani ya Kenya ambao wataingia nchini kufanyiwa vipimo kwa haraka na majibu kupatikana kwa wakati.

Alisema uwepo wa maabara hiyo utaondoa changamoto iliyokuwepo ya kusafirisha sampuli kwenda kwenye maabara nyingine ambapo ilikuwa inasababisha ucheleweshwaji wa majibu na wakati mwingine vipimo vilikuwa vinachelewa.

"Kwa niaba ya Serikali, tunawashukuru wenzetu wa Ujerumani kwa kutusaidia katika sekta ya Afya, kama mnavyofahamu hospitali hii ilijengwa na wajerumani miaka 100 iliyopita lakini bado wanaendelea kutoa fedha nyingi katika kusaidia sekta ya afya nchini ikiwemo hospitali yetu ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga Bombo wanatupatia fedha kwa ajili ya kuimarisha afya ya uzazi, mama na mtoto pamoja na mapambano dhidi ya ugonjwa wa UVIKO - 19". Alisema Mhe. Ummy.

Alisema kuzinduliwa kwa kituo hicho cha kupima sampuli za UVIKO - 19 kutasaidia kuokoa muda kwani awali ilikuwa inawalazimu sampuli zinazochukuliwa hospitali ya Bombo kwenda kupimwa Dar es Salaam kwenye maabara ya Taifa na baada ya masaa 48 ndio majibu kupatikana ambapo sasa majibu yatakuwa yanapatikana ndani ya masaa 8 na kuwarahisishia wanaosafiri kwenda nje ya nchi kupata majibu kwa haraka zaidi.

Waziri Ummy alisema pia fedha walizitoa zitatumika kwa ajili ya kuimarisha mapambano dhidi ya UVIKO -19 na ndio maana katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa Bombo wamefungua kituo cha kupima sampuli za UVIKO -19 kwa kutumia kipimo hicho.

Awali, akizungumza Waziri wa Ushirikiano wa Uchumi na Maendeleo kutoka Serikali ya Ujerumani, Dkt. Barbel Kofler alisema kuwa wakazi wa Tanga pamoja na wageni kutoka nje sasa wataweza kutumia maabara hiyo kwa ajili ya vipimo vya UVIKO -19.

Alisema wanajisikia furaha kuona kituo hiki cha kupimia sampuli za UVIKO -19 kinaanza kufanya kazi kwa ajili ya kuimarisha afya ya jamii ya watu wa Tanga na ni muhimu sana kwa Serikali ya Ujerumani kuendelea kusaidia sekta ya afya katika mapambano dhidi ya magonjwa mbalimbali ya mlipuko.

Alieleza kwa sababu wote hatuko salama muda wowote hivyo wanapaswa kushirikiana kusaidia katika kuimarisha afya ya jamii kwa ujumla kwa Tanzania na ulimwengu mzima pia

Dkt. Kofler alisema, mbali na fedha hizo wamesaidia kuwajengea uwezo wataalamu wa afya katika kutoa huduma bora huku wakitoa Dola za kimarekani 15.3 kwa ajili ya kusaidia afya ya mama na mtoto na wasichana ili kupambana, kupunguza au kutokomeza kabisa vifo vitokanavyo na uzazi.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Maabara Kuu ya Taifa ya Afya ya Jamii,  Medard Beyanga alisema kuwa  Serikali inaendelea kuziimarisha maabara zote hapa nchini kwa ajili ya kupelekea huduma karibu na  wananchi  ambapo baadhi ya vituo hapa nchini vimeanza kufunguliwa  ikiwemo kilichopo katika  Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Tanga  Bombo.

Alisema kwamba hivi sasa wanaendelea na mpango wao wa kuziimarisha maabara  za upimaji wa UVIKO -19 na Serikali inafanya jitihada za  kuongeza upimaji  ili kupeleka huduma karibu na wananchi kuliko kusubiri majibu kutoka Dar es salaam kwenda Maabara Kuu ya Taifa, na hii maabara haitakuwa ya kupima UVIKO -19 bali itapima na magonjwa mengine.

Aidha, Serikali ya Ujerumani pia imeendelea kuwa na mchango mkubwa hapa nchini kupitia sekta ya afya ambapo inasaidia kulipia bima ya afya na mtoto inayotambulika kama 'Tumaini la mama', kuchangia mapambano dhidi ya kifua kikuu pamoja na malaria.

“Serikali ya Ujerumani imedhamini miradi ya afya nchini Tanzania kwa gharama ya Dola za kimarekani za zaidi ya Shilingi bilioni 7 ikihusisha miradi ya mama na mtoto na Uviko 19”, alisema

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi