Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

DAWASA yajipanga kuongeza mapato yake kufikia Shilingi Bilioni 12 kwa mwezi
Oct 20, 2018
Na Msemaji Mkuu

 

Na; Frank Mvungi

Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA)imejiwekea malengo ya kukusanya shilingi bilioni 12 kila mwezi ikiwa ni sehemu ya matokeo ya maboresho yanayofanyika ili kuongeza tija katika huduma zinazotolewa na Mamlaka hiyo.

Akizungumza katika Kipindi cha “TUNATEKELEZA” kinachorushwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC),Waziri wa Maji Prof. Makame Mbarawa amesema kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kuwa wananchi wanafikiwa na huduma ya majisafi na salama katika maeneo yote hapa nchini ikiwemo Jiji la Dar es Salaam na viunga vyake.

“Kuunganishwa kwa DAWASCO na DAWASA kunalenga kuongeza tija katika huduma zinazotolewa kwa wananchi na kupunguza gharama za uendeshaji hali itakayosadia fedha zinazookolewa kuelekezwa kuboresha huduma kwa wananchi hasa wanaoishi maeneo ya pembezoni”. Alisisistiza Mhe. Prof. Mbarawa

Akifafanua amesema kuwa asilimia 35 ya mapato yote ya DAWASA yanayokusanywa yataelekezwa katika kupeleka huduma ya maji kwa wananchi walio maeneo ya pembezoni.

Aliongeza kuwa DAWASA imeunda kikosi kazi cha kushughulikia tatizo la upotevu wa maji katika Jiji la Dar es Salaam kwa kuimarisha miundombinu  iliyopo hali itakayosaidia kuimarika kwa huduma ya maji katika maeneo yote yanayohudumiwa na Mamlaka hiyo.

 Kwa sasa  DAWASA imejikita katika kuhakikisha kuwa huduma zinazotolewa kwa wananchi  zinaendana na kasi ya Serikali ya Awamu ya Tano inayosisitiza katika kutoa huduma bora kwa  na kwa wakati ambapo Mamlaka hiyo imeweka mfumo unaowawezesha wananchi kuwasilisha taarifa pale ambapo kuna changamoto kupitia namba  0800110064.

Lengo la Mamlaka hiyo kukusanya Bilioni 12 kila mwezi linaonesha juhudi za makusudi zinazochukuliwa ambapo awali  jukumu la kukusanya mapato lilikuwa chini ya DAWASCO ambayo sasa imeunganishwa na DAWASA na hivyo majukumu yote ya DAWASCO kuhamishiwa DAWASA, DAWASCO ilikuwa ikikusanya kati ya biloni 7 hadi 8 kwa mwezi.

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi