Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Wekeni Juhudi Katika Masomo ya Hisabati na Sayansi - Dkt. Judith, Mhadhiri Nelson Mandela
Mar 22, 2024
Wekeni Juhudi Katika Masomo ya Hisabati na Sayansi - Dkt. Judith, Mhadhiri Nelson Mandela
Mhadhiri wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela na Mratibu wa Uhusiano wa Kitaaluma na Viwanda katika Mifumo iliyopachikwa na Simu (EMoS), Dkt. Judith Leo akiwaelekeza matumizi ya kompyuta wanafunzi wa shule ya msingi Nganana iliyopo Arumeru jijini Arusha wakati wa ziara ya uenezi na huduma kwa jamii shuleni hapo Machi 21, 2024.
Na Lorietha Lawrence

Mhadhiri wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela na Mratibu wa Uhusiano wa Kitaaluma na Viwanda katika Mifumo iliyopachikwa na Simu (EMoS), Dkt. Judith Leo amewataka wanafunzi wa shule ya msingi Nganana na Nambala kuweka juhudi katika masomo ya Sayansi na Hisabati kwa kuwa siyo magumu kama ambavyo wanafikiri bali juhudi binafsi na kupenda somo kunaweza kuwafanya wafaulu vyema.

 

Dkt. Judith ameyasema hayo Machi 21, 2024 alipotembelea shule hizo akiwa ameongozana na wanafunzi wa Shahada ya Umahiri (CEMoS) wa Kituo cha Ubora cha TEHAMA Afrika Mashariki (CENIT@EA) katika ziara ya uenezi na huduma kwa jamii katika shule hizo mbili zilizopo Arumeru jijini Arusha lengo likiwa ni kuhamasisha umuhimu wa kuweka mkazo katika masomo hayo.

Wanafunzi wa Shule ya Msingi Nambala iliyopo Arumeru jijini Arusha wakiwasikiliza wanafunzi wa Shahada ya Umahiri katika Mifumo Iliyopachikwa na Simu (EMoS) kutoka kituo cha Ubora cha TEHAMA Afrika Mashariki kilichopo Katika Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela walipokuwa wakitoa elimu kwa vitendo walipotembelea shule hiyo Machi 21, 2024.

Aidha, wanafunzi wa Shahada ya Umahiri katika Mifumo iliyopachikwa na Simu (EMoS) walitoa elimu kwa vitendo ya namna ya kutumia vifaa mbalimbali vya kisayansi ikiwemo kompyuta, vifaa vya maabara katika kutambua matatizo mbalimbali yanayoikabili jamii ili kuwapatia ufumbuzi wa kutatua changamoto hizo.

Mhadhiri Dkt. Judith Leo na wanafunzi wa Shahada ya Umahiri katika Mifumo Iliyopachikwa na Simu (EMoS) kutoka Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela wakiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi wa shule ya msingi Nambala mara baada ya kutoa elimu kwa vitendo katika masuala ya Sayansi na Hisabati Machi 21,2024 jijini Arusha.

Naye, Mwanafunzi wa Shahada ya Umahiri katika Mifumo Iliyopachikwa na Simu (EMoS), Seth Odwar kutoka nchini Kenya amewahimiza wanafunzi hao kuzingatia somo la Hisabati ambalo wengi huhisi halina manufaa katika kozi nyingine na kuongeza kuwa sayansi ni muhimu katika kutatua changamoto za jamii.

Mhadhiri na wanafunzi wa Shahada ya Umahiri katika Mifumo Iliyopachikwa na Simu (EMoS) kutoka Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela wakiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi wa shule ya msingi Nganana mara baada ya kutoa elimu kwa vitendo katika masuala ya Sayansi na Hisabati Machi 21, 2024 jijini Arusha.

Akizungumza kwa niaba ya wanafunzi wenzake, Jackline Mushi ameishukuru Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela kwa kutoa hamasa kwa vitendo pamoja na kuwajengea uwezo katika matumizi ya vifaa vya kisayansi ikiwemo kompyuta.

 

Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela inatekeleza majukumu yake katika misingi mitano (5D Business Modal) ambapo mojawapo ya msingi huo ni Uenezi na Huduma kwa Jamii (Outreach na Community Engagement).

 

 

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi