Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Watumishi wa Umma Watakiwa Kutumia Majengo ya Serikali Kutatua Kero za Wananchi
Jul 24, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Mpango amewaasa watumishi wa umma kutumia majengo ya Serikali kuhudumia na kutatua kero za wananchi kwa kufuata sheria na taratibu za utumishi wa umma ikiwa ni pamoja na kujiepusha na vitendo vya rushwa na ufisadi.

Makamu wa Rais amesema hayo leo tarehe 22 Julai, 2022  alipozindua jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Mpindwe mkoani Katavi, Jengo lililogharimu Shilingi bilioni 2.9.

 Amewaasa watendaji na watumishi wote wa halmashauri kuhakikisha fedha zinazopelekwa na Serikali katika maeneo yao zinatumika kikamilifu na kwa lengo lililokusudiwa. Amesema umefika wakati wa watendaji kuacha kufanya kazi kwa mazoea badala yake wanapaswa kutoa huduma zilizo bora kwa kujitoa na kwa upendo mkubwa.

Aidha, Makamu wa Rais ameiagiza Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kuharakisha uhakiki  na kufanya fidia kwa wananchi wanaostahili ili kuendelea na utekelezaji wa mradi wa barabara ya Kibaoni – Majimoto – Inyonga ambayo imekua changamoto kwa muda mrefu. Pia amesema Serikali itashughulikia kikamilifu suala la changamoto ya maji katika halmashauri hiyo na kuagiza wizara ya maji kuhakikisha mradi wa kutoka kata ya Majimoto unakamilika kufikia Novemba mwaka huu.

Kwa upande wake Naibu Waziri Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Mhe. Dkt. Festo Dugange amesema Serikali tayari imepeleka bilioni 3.4 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe na tayari wananchi wameanza kupata huduma katika hospitali hiyo. Aidha ameongeza kwamba Serikali ya Awamu ya Sita imetoa Shilingi  milioni 300 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la magonjwa ya dharura katika halmashauri hiyo.

Mbunge wa Jimbo la Kavuu ambaye pia ni Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Geoffrey Pinda ameiomba serikali kuanzisha wilaya ya kipolisi katika halmashauri hiyo pamoja na ujenzi wa gereza ili kuwasaidia wananchi kupata haki zao kwa ukaribu zaidi.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mheshimiwa Mwanamvua Mrindoko ameishukuru serikali kwa ujenzi wa majengo saba ya utawala katika mkoa huo ambayo yatawezesha watumishi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Awali, Makamu wa Rais, Dkt. Philip Mpango aliweka jiwe la msingi katika kituo cha afya Kibaoni Halmashauri ya Mpimbwe ambapo amesema serikali itaendelea kusogeza karibu na wananchi huduma zote muhimu zikiwemo huduma za afya. Amewapongeza watendaji wa halmashauri hiyo kwa kutumia fedha za ndani katika kutekeleza mradi huo. Makamu wa Rais amewaasa wahudumu wa afya kuwahudumia wananchi kwa utaalamu na kwa kufuata maadili ya kazi yao.

Makamu wa Rais ameagiza kituo hicho cha afya kukamilika mwezi Septemba mwaka huu na tarehe Mosi Oktoba kuanza kutoa huduma kwa wananchi wa eneo hilo.

Makamu wa Rais Mhe. Dkt. Philip Mpango yupo ziarani mkoani Katavi kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo pamoja na kusikiliza kero na changamoto za wananchi wa mkoa huo.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi