Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Viongozi Wahamasika Kuhama Ngorongoro
Jun 22, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Na Mwandishi Wetu – NGORONGORO

Viongozi wa Watanzania wanaoishi kwenye Hifadhi ya Ngorongoro wamehamasika kuhama kwa hiari kutoka kwenye hifadhi hizo na kuhamia kwenye makazi waliyoandaliwa na Serikali yaliyopo katika Kijiji cha Msomera, Wilaya ya Handeni mkoani Tanga. 

Hayo yamedhihirika leo ndani ya eneo hilo pindi wanahabari walipowatembelea viongozi waliohamasika akiwemo Diwani wa Kata ya Eyasi, Mhe. Augustino Rumay, Diwani wa Viti Maalum Tarafa ya Ngorongoro, Mhe. Veronica Mifurda na Kiongozi wa Kimila wa Jamii ya Wadatoga (Soguchan), Ndg. Kwandaja Gidamusungu.

Mhe. Rumay amesema kwamba ameamua kuhama ili kupisha uhifadhi wa eneo hilo unaofanyika kwa maslahi mapana ya Taifa.

“Nimefanya uamuzi huo baada ya kuongea na familia yangu na kuridhia kupokea ombi la serikali, hakuna ulazima wa aina yoyote,” amedokeza.

Kwa upande wake, Mhe. Mifurda ameeleza kuwa ameamua uamuzi wa kuhama kutoka kwenye eneo hilo kwa sababu anataka kuanza maisha mapya ambayo ni bora ukilinganisha na maisha anayoishi sasa.

“Nimeridhia kujiandikisha kwa sababu maisha tunayoishi huku ni maisha yasiyoridhisha, mahitaji wanayopata wenzetu sisi hatuyapati, ni afadhali niende nikawe huru nipate hati miliki yangu ndio maana nikaridhia kwenda kujiandikisha ili niwe huru na niwe na amani,” amehabarisha.

Naye, Ndg. Gidamusungu amearifu kwamba tayari amejiandikisha kwenye orodha ya watakaohama kwa sababu huko anapohamia ataweza kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi.

“Nimekuwa nikiihamasisha jamii yangu ya Datoga ili tuhame, wengine wanakubali lakini wale wasioonesha utayari kwa wakati huu nimekuwa nikiwaelimisha kwamba twende kwenye maisha mengine, sio kuishi ndani ya eneo la hifadhi,” ameeleza. 

Kila kaya inayohamia katika Kijiji cha Msomera inapewa ekari tatu kwa ajili ya makazi na ekari tano kwa ajili ya kilimo na ufugaji. 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi