Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Tume ya Madini Yajipanga Kufikia Asilimia 10 Mchango Pato la Taifa
Mar 04, 2025
Tume ya Madini Yajipanga Kufikia Asilimia 10 Mchango Pato la Taifa
Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani M. Lwamo, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio na mwelekeo wa tume hiyo katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya awamu ya sita tarehe 4 Machi, 2025, katika ofisi za Idara ya Habari - MAELEZO, Dodoma.
Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO

Kutokana na kuimarika kwa Sekta ya Madini nchini, muelekeo wa Tume ya Madini ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2025, mchango wa sekta hiyo katika Pato la Taifa ufikie asilimia 10 au zaidi.

Lengo la sekta ya madini kuchangia asilimia 10 katika pato la Taifa limebainishwa pia kwenye Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025, Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya Mwaka 2020 na Mpango Mkakati wa Tume ya Madini wa Mwaka 2024/2025-2025/2026.

Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, amebainisha lengo hilo leo Machi 04, 2025, katika ukumbi wa Idara ya Habari- MAELEZO jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Tume hiyo katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Amesema kuwa katika kuhakikisha azma hiyo inafikiwa, Tume imeandaa mikakati mbalimbali itakayowezesha kuwepo kwa usimamizi wa shughuli za madini ambazo ni endelevu na zenye tija kwa Taifa na jamii kwa ujumla.

“Baadhi ya mikakati hiyo iliyowekwa na Tume ni kuendelea kuimarisha usimamizi na udhibiti katika maeneo ya uzalishaji wa madini ujenzi na madini ya viwandani kwa kuongeza wakaguzi wasaidizi wa madini ujenzi (AMAs), vitendea kazi (PoS) pamoja na kushirikisha mamlaka nyingine za Serikali zinazosimamia na kutumia rasilimali hizi, zikiwemo halmashauri, Polisi, TARURA na TANROADS, uboreshaji na usimamizi thabiti wa mfumo wa utoaji wa leseni za madini pamoja na kuimarisha mazingira ya uwekezaji kwa wachimbaji wa madini”, amesema Mhandisi Lwamo.

Kwa mujibu wa Lwambo, mikakati mingine ni kuimarisha udhibiti wa biashara haramu ya madini hususan utoroshaji wa madini kwa kuhamasisha umuhimu wa kutumia masoko na vituo vya madini nchini, kuimarisha vituo vya ukaguzi katika maeneo ya mipakani, bandarini pamoja na viwanja vya ndege, kuimarisha ukaguzi katika shughuli za uchimbaji katika migodi, kuimarisha ofisi za RMOs, maabara na MROs katika maeneo mbalimbali ya uzalishaji hapa nchini pamoja na kuimarisha shughuli za tafiti zinazohusiana na utambuzi wa vyanzo vipya vya mapato yatokanayo na rasilimali za madini.

Sekta ya Madini ni miongoni mwa sekta muhimu katika kukuza uchumi na kuleta maendeleo ya kijamii na Taifa kwa ujumla.

Mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita katika Sekta hiyo, yametokana na uongozi makini na imara wa Serikali chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Aidha, kuimarika kwa sekta hiyo kumesaidia kuongeza mapato ya Serikali na kukua kwa mchango wa sekta hiyo nchini.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi