Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Rais Samia Atoa Bilioni 500 Ununuzi wa Vifaa vya Kuhudumia Mizigo Bandari ya Dar es Salaam
May 17, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Mkurugenzi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari nchini (TPA), Erick Hamisi akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kumalizika kwa mkutano wa wadau wa bandari kilichofanyika leo Jijini Tanga

Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu imetoa Shilingi bilioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kuhudumia mizigo ili kuongeza ufanisi katika Bandari ya Dar es Salaam.

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari nchini (TPA), Erick Hamisi wakati wa mkutano wa wadau wa bandari unaofanyika Jijini Tanga ambapo alisema uwekezaji huo unaokwenda kufanyika katika bandari hiyo ni mkubwa ambao utafungua fursa kwa nchi na maziwa makuu kwa matumizi ya bandari hiyo.

Alisema kuwa kuna mradi wa ujenzi wa bandari kavu ya Kwara ambapo watapeleka mizigo ya nje katika nchi za Maziwa Makuu (Transit) baada ya Serikali kuwekeza fedha hizo ambazo pia zitatumika kununulia vifaa ili kuwezesha ufanisi huo.

Wadau wa Bandari wakisikiliza mada mbalimbali zilizotolewa katika warsha ya wadau hao iliyoandaliwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari nchini (TPA) na kufanyika jijini Tanga.

“Tutakuwa na ujenzi wa bandari ya nchi kavu ya kwara, isitoshe Serikali ya Awamu ya Sita imewekeza kiasi cha Shilingi bilioni 500 kwa mara moja uwekezaji ambao haujawahi kufanyika kwa mara moja, hii inaonesha Mhe. Rais amedhamiria kuifanya bandari yetu ifanye kazi kwa ufanisi,” alisema Hamissi.

Mkurugenzi huyo alisema uwekezaji unaofanyika kwa sasa katika miundombinu ya reli, Bandari na kwenye maziwa inaonesha kwamba nchi zote zinazotuzunguka hazitakuwa na chaguo lingine bali kutumia bandari ya Dar es salaam.

Mkurugenzi huyo alisema mkutano unaofanyika mjini Tanga uliowakutanisha wadau wa bandari haujawahi kufanyika hivyo, utatoa fursa kwa wadau kujadili vikwazo na fursa zilizopo katika kuongeza ufanisi zaidi ya bandari zilizopo hapa nchini.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Wakala wa meli nchini (TASAC), Kaimu Abdi Mkeyenge alisema kwamba wadau wamekutanishwa pamoja ili kutazama changamoto wanazokutana nazo kisha waweze kuzipatia majawabu ya mapendekezo ya kuyafanyia kazi kwa pamoja.

Alisema warsha hiyo itatazama changamoto mbalimbali ambazo zinaipata bandari ya Dar es Salaam na fursa zilizopo na kutoa mapendekezo ya kuboresha ikiwemo bandari ya Tanga.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika la Reli nchini (TRC), Masanja Kadogosa, alisema mkutano huo wa wadau utasaidia kuongeza fursa za usafirishaji mizigo utakaofanywa na shirika hilo ambalo limefanya ukarabati wa reli yake ili kuweza kuhudumia nchi za maziwa makuu.

Naye Mtendaji Mkuu wa Wasafirishaji nchini (TAT), Ashraf Khan alisema wao kama wasafirishaji wanaiomba bandari iwasaidie maroli yao yanayobeba mizigo bandarini yaweze kutoka kwa wepesi ili meli zinazoingia bandarini zichukue muda mfupi kukaa bandarini.

Awali akifungua warsha hiyo ya siku mbili, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Adam Malima, aliwataka wajumbe wa mkutano huo ikiwemo uongozi wa Bandari kutazama changamoto hizo na kuzipatia majawabu ili bandari ya Dar es salaam iweze kushindana na bandari nyingine zilizopo katika ukanda huu.

Alisema wanapofikiria kuondoa changamoto katika bandari ya Dar es salaam wafuate maelekezo yanayotolewa na Rais Samia ili waweze kuongeza tija lakini pia kushindana na bandari za Beira nchini Msumbiji pamoja na ile ya Mombasa nchini Kenya.

“Kuweni mfano wa kile ambacho Rais wetu anachohubiri kuitaka bandari ifanye kazi kwa ufanisi, tusiwe watu wa kuiangusha bandari, tuifanye ifanye vizuri kushindana na bandari nyingine,” alisema Mkuu wa mkoa huyo.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi