Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dkt. Hussein Mwinyi na Mkewe Bi. Mariam Mwinyi ni miongoni mwa viongozi waliowasili nyumbani kwa Hayati Edward Lowassa jijini Dar es Salaam kutoa mkono wa pole kwa familia ambapo amesema yeye na wananchi wa Zanzibar wameupokea kwa masikitiko makubwa msiba huo.
Rais Mwinyi amewasili nyumbani hapo leo Februari 12 na kutoa pole kwa familia ambapo pia amesema yeye ni miongoni mwa viongozi waliowahi kufanya kazi na Lowassa wakati wa uongozi wa Rais wa awamu ya tatu Hayati Benjamini Mkapa na kwamba anaungana na watanzania wote katika kipindi hiki cha majonzi.
“Nimekuja hapa kutoa pole kwa familia ya Waziri Mkuu Mstaafu Hayati Edward Lowassa, nimekuja hapa kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, na wananchi wote za Zanzibar ,tumekuja kutoa pole kwa mwenzetu aliyetangulia mbele ya haki, kipindi hiki ni cha majonzi na sisi kama binaadamu tuna wajibu wa kufarijiana” amesema Dkt. Mwinyi.
Amesema katika enzi za uhai wakeHayati Lowassa amefanya kazi kubwa kwenye maendeleo ya taifa na kwamba atakumbukwa kwa mazuri mengi.
“Marehemu Lowassa nimefanya nae kazi kwa pamoja tukiwa mawaziri wote kwa pamoja, tukiwa chini ya Hayati Mzee Mkapa, hivyo msiba huu tumeupokea kwa masikitiko makubwa na leo tupo hapa kutoa mkono wa pole kwa niaba ya wananchi wote za Zanzibar”, amesema Dkt. Mwinyi.