Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Rais Dkt. Mwinyi Azungumza na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Oman
Sep 23, 2024
Rais Dkt. Mwinyi Azungumza na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Oman
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akizungumza na mgeni wake Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Oman anayeshughulikia Masuala ya Utawala na Fedha, Mhe. Khalid Almuslahi (kulia kwa Rais). Kulia kwa Waziri wa Mambo ya Nje ni Balozi Mdogo wa Oman anayefanyia kazi zake Zanzibar, Mhe. Said Salim Al Sinawi. Mazungumzo hayo yamefanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo 23-9-2024.
Na Ikulu - Zanzibar

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema itajenga hospitali kubwa ya Mkoa maeneo ya Mahonda, Wilaya ya Kaskazini B Mkoa wa Kaskazini Unguja ambayo itafadhiliwa na Serikali ya Oman.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi ameyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipokutana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Oman anayeshughulikia Utawala na Fedha, Khalid Almuslahi.

Dkt. Mwinyi amesema ujenzi wa hospitali hiyo ni muhimu kwa dhamira ya Serikali ya kuwa na hospitali kubwa kwa kila Mkoa ili kuwafikishia wananchi huduma bora karibu na makazi yao na kupunguza msongamano kwenye hospitali ya Rufaa ya Mnazi Mmoja.

Rais Dkt. Mwinyi ameipongeza Serikali ya Oman kwa kushiriki kikamilifu kwenye miradi ya maendeleo hapa nchini kwa taasisi mbalimbali za nchi hiyo kuiunga mkono Zanzibar kiufundi na kitaalamu.

Dkt. Mwinyi alimuhakikishia Naibu Waziri huyo kwamba uhusiano uliopo baina Zanzibar na Oman upo imara, hivyo miradi ya ushirikiano inayoendelea itaweka alama zaidi katika kudumisha uhusiano wa diplomasia baina ya pande mbili hizo.

Akizungumzia Mji Mkongwe wa Zanzibar, alisema kuwa ni eneo muhimu la urithi, linalohitaji kuendelezwa wakati wote, hivyo juhudi zinazofanywa na Serikali ya Oman ya kuukarabati na kuuimarisha ni kuunga mkono juhudi za Serikali kuinua uchumi wa nchi.

Alisema, Mji Mkongwe mbali ya kuwa kivutio cha utalii pia ni eneo muhimu la kukuza Uchumi na utamaduni wa Zanzibar na Serikali itaendelea kuchukua juhudi mbalimbali za kuutunza mji huo. 

Serikali ya Oman katika kuendeleza ushirikiano wake na Zanzibar inafadhili miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa hospitali, ukarabati wa Mji Mkongwe, huduma za maji na umeme na elimu.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi